Wakimbizi wapenzi wa jinsia moja Kenya wahofia usalama wao kambini

Wanaomba kuhamishwa kwa kile walichokitaja kuwa ni ongezeko la ubaguzi na unyanyasaji.

Muhtasari

•Mmoja wa wakimbizi hao, ambaye aliomba jina lake lisitajwe kutokana na hofu ya kutokea mzozo zaidi, aliambia BBC "hatujisikii salama tena kambini".

•Wiki iliyopita kulikuwa na maandamano ya makundi ya LGBT katika kambi hiyo.

Kumeripotiwa visa vya unyanyasaji wa wakimbizi wanaoshiriki mapenzi ya jinsia katika kambi hiyo katika miaka michache iliyopita.
Kumeripotiwa visa vya unyanyasaji wa wakimbizi wanaoshiriki mapenzi ya jinsia katika kambi hiyo katika miaka michache iliyopita.
Image: BBC

Wakimbizi wanaoshiriki mapenzi ya jinsia moja (LGBT) katika kambi moja kubwa nchini Kenya wanaomba kuhamishwa kwa kile walichokitaja kuwa ni ongezeko la ubaguzi na unyanyasaji unaofanywa na wakimbizi wengine dhidi yao katika kambi hiyo kwa sababu ya mwelekeo wao wa kijinsia.

Mmoja wa wakimbizi hao, ambaye aliomba jina lake lisitajwe kutokana na hofu ya kutokea mzozo zaidi, aliambia BBC "hatujisikii salama tena kambini".

Kakuma inaendeshwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) na ni mojawapo ya kambi kubwa zaidi za wakimbizi nchini Kenya, inayohifadhi maelfu ya wakimbizi wa ndani, pamoja na wale kutoka nchi jirani.

Wiki iliyopita kulikuwa na maandamano ya makundi ya LGBT katika kambi hiyo, ambayo yalilalamikia unyanyasaji na unyanyasaji dhidi yao, ambayo ilisababisha kukamatwa kwa muda kwa watu 18, ugomvi, na matumizi ya gesi ya machozi.

Wote waliozuiliwa waliachiliwa siku iliyofuata baada ya maafisa wa UNHCR kujadiliana kuachiliwa kwao.

"Tumechoshwa, Kakuma si salama tena kwetu sisi wanachama wa jumuiya ya LGBTQI. Tunatishiwa. Tumetoa malalamiko kwa UNHCR na hakuna hatua iliyochukuliwa," alisema mkimbizi huyo.

Wanadai kuwa ubaguzi na unyanyasaji huo umewafanya kushindwa kupata huduma za kijamii kama vile elimu na matukio yanayofanyika katika kambi hiyo kwa sababu hawaruhusiwi kujumuika jamii nyingine.

Msemaji wa UNHCR aliiambia BBC kwamba shirika hilo limekuwa likifanya kazi na jumuiya ya LGBT katika kambi hiyo ili kuwahakikishia usalama wao kwa kuongeza doria ya polisi wanakoishi na kufanya kazi, pamoja na watu wa kujitolea kusaidia na kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya usawa na ulinzi wa haki za watu hao.