Rais William Ruto ametia saini mswada wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka, IEBC wa 2024 na kuwa sheria.
Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa KICC Jumanne 9,Julai 2024,huku viongozi wa Azimio Raila Odinga na aliyekuwa makamu wa Rais Kalonzo Musyoka wote walikuwepo wakati wa utiaji saini huo.
Kwenye taarifa yake rais Ruto alisema ;
"IEBC inabaki kuwa nguzo ya demokrasia yetu inayohusika na kusimamia uchaguzi wa kawaida katika viwango mbalimbali na kuhakikisha mzunguko wetu wa uchaguzi unasimamiwa kwa uwazi na kusimamiwa kwa njia isyoegemea upande wowote kwa ufanisi ,kwa usahihi na kwa uwajibikaji."
Ili kusaidia kurejesha imani ya wananchi katika mfumo wa uchaguzi,Rais alisema kuwa;
"Tumeweza kuleta pamoja vyama vyote vya kisiasa na jamii ya kiraia ili kuhakikisha kuwa tume mpya ya IEBC itakuwa ya haki na yenye uwazi."
Rais alisema kuwa amepunguza uwakilishi wa kamati ya huduma za bunge kwenye jopo la uteuzi kutoka wanachama wanne hadi wawili ili kuongeza wanachama kutoka kamati ya uratibu wa vyama vya kisiasa.
Mswada huo uliopitishwa na bunge unatokana na mapendekezo ya ripoti ya kamati ya kitaifa ya majadiliano (NADCO).
Sheria hiyo mpya itaweka mfumo wa usimamizi wa uchaguzi nchini, ikiwa ni pamoja na kuandaa njia ya uteuzi wa makamishna wapya wa IEBC.
Rais amekuwa akishinikizwa kutia saini mswada wa IEBC huku baadhi ya wakenya wakiitaka kuwarudisha nyuma wabunge wao kwa ajili ya kupiga kura kuunga mkono mswada wa fedha wa 2024 uliopingwa.
Viongozi wa upinzani na baadhi ya makasisi wamekuwa wakitaka kutiwa saini kwa mswada huo ili kuwezesha kuundwa upya kwa wakala wa uchaguzi.