logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mkenya akamatwa akishirikiana na Mchina nchini Tanzania kuiba vifaa vya ujenzi wa SGR

Washukiwa hao ni pamoja na watu kutoka China, Kenya, na Tanzania, ambao baadhi yao walikuwa wafanyakazi wa kampuni ya ujenzi wa reli ya Uturuki, Yapi Merkez.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari19 December 2024 - 11:24

Muhtasari


  • Kampuni hiyo inayodaiwa kumilikiwa na watu kutoka China na Kenya, ilikutwa na waya za shaba zenye uzito wa kilo 882 mali ya Shirika la Reli Tanzania (TRC).
  • "Natoa onyo kwa yeyote anayepanga kuhujumu SGR na miundombinu mingine ya umeme kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi yao," Kamanda Hyera alionya.



POLISI wa kitengo cha shirika la reli nchini Tanzania wamewatia mbaroni zaidi ya watu 13 wakishukiwa kuhusika katika wizi wa vifaa vya ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR nchini humo.


Kwa mujibu wa kamanda wa kitengo hicho cha polisi, Hyera Gallus, watu hao walikamatwa wakiwa na vifaa hivyo kinyume cha sheria na kushtakiwa kwa kosa la uhujumu wa uchumi na wizi wa nyaya za shaba.


Kamanda wa Polisi wa Shirika la Reli, Gallus Hyera, alionyesha waya zilizoibiwa zilizookotwa katika maeneo mbalimbali.


 Alifichua kuwa washukiwa hao ni pamoja na watu kutoka China, Kenya, na Tanzania, ambao baadhi yao walikuwa wafanyakazi wa kampuni ya ujenzi wa reli ya Uturuki, Yapi Merkez.


Kati ya waliokamatwa, wanane walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha mkoani Pwani, huku watano wakifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni, Dar es Salaam, wote wakikabiliwa na mashtaka yanayofanana ya uhujumu uchumi.


Kamanda Hyera alieleza kuwa kukamatwa kwa watu hao kunatokana na operesheni kubwa ya kiintelejensia iliyowezesha polisi kupata nyaya zilizoibwa na vifaa vingine vya miundombinu ya reli.


Miongoni mwa mshukiwa huyo ni fundi wa umeme aliyeajiriwa na Yapi Merkez, ambaye kwa mujibu wa polisi alihusika katika kukata na kuiba nyaya hizo.


Aidha alifichua kuwa wamiliki wa Kampuni ya African Light Investment inayofanya shughuli zake Visiga Wilaya ya Mlandizi pia walikamatwa.


Kampuni hiyo inayodaiwa kumilikiwa na watu kutoka China na Kenya, ilikutwa na waya za shaba zenye uzito wa kilo 882 mali ya Shirika la Reli Tanzania (TRC).


"Natoa onyo kwa yeyote anayepanga kuhujumu SGR na miundombinu mingine ya umeme kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi yao," Kamanda Hyera alionya.


Aliitaka jamii kuchukua jukumu kubwa katika kulinda miundombinu ya reli na kutoa taarifa kwa vitendo vya uharibifu au uhalifu.


Mwezi mmoja uliopita, Jeshi la Polisi mkoani Dodoma liliwakamata watu sita kwa tuhuma za kuharibu na kuiba waya za shaba kwenye miundombinu ya Reli ya Standard Gauge (SGR) katika wilaya za Mpwapwa na Bahi, mkoani Dodoma.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma (RPC) George Katabazi alithibitisha kukamatwa kwa watu hao na kufafanua matukio hayo.


 



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved