

Mamia ya wakaazi wa Bungoma waliingia barabarani katika maandamano ya amani kupinga vitisho vya kumtimua Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangula.
Waandamanaji hao wakiwemo waendesha bodaboda walilaani wabunge wa upinzani kwa kutaka Wetangula aondolewe kwa madai ya upendeleo katika shughuli za bunge.
Walimtaka Rais William Ruto kumlinda, wakitaja uaminifu wake na jukumu lake katika kuendeleza ajenda ya Kenya Kwanza.
"Wetangula ni mwana wetu. Alisaidia kuwasilisha kura ya Magharibi mwa Kenya kwa Ruto mwaka wa 2022. Wanaoshinikiza kuondolewa kwake mashtaka wanapaswa kuheshimu mchango wake," mmoja wao alisema.
Waandamanaji hao walikariri ziara ya Ruto mjini Bungoma mwaka wa 2022, ambapo aliidhinisha Wetangula kuwa Spika, na kuhakikishia kuwa Kenya Kwanza ilikuwa na nambari za kumchagua.
"Tuna idadi katika Bunge, na bila shaka, Wetang’ula atakuwa Spika wetu," Ruto alikuwa ametangaza.
Wakazi hao walishutumu wabunge wa upinzani kwa kuvuruga Bunge na kuwataka waunge mkono ajenda ya maendeleo ya serikali badala yake.
Maandamano hayo yalimalizika kwa amani, huku wakaazi wakionya kuwa wataandaa maandamano zaidi ikiwa vitisho vya kushtakiwa vitaendelea.
Maandamano hayo yalijiri baada ya Mbunge wa Starehe, Amos Mwago kutishia kuwasilisha hoja ya kumshtaki Spika iwapo atashindwa kujiuzulu.
Mwago alidai kuwa Wetangula amesimamia kwa uzembe koti la uongozi muhimu na amewajibika kwa baadhi ya sababu kuu za machafuko ya umma, ikiwa ni pamoja na Mswada wa Fedha wa 2024 ambao ulisababisha migomo nchi nzima.
Mbunge huyo alishikilia kuwa kufuatia uamuzi wa Mahakama ya Juu uliotaja jukumu la Wetangula kama Spika na kiongozi wa Ford Kenya kuwa kinyume na katiba, bado hafai kuwa kwenye usukani wa uongozi wa Bunge.
Wiki iliyopita, Wetangula alitoa uamuzi tata kwa kutangaza Kenya Kwanza kuwa chama kikuu katika Bunge licha ya Mahakama Kuu kutangaza kwamba haikuwa chama cha wengi.