
Maelfu ya waandamanaji, ambao hapo awali walikuwa wamezuiwa kuingia kwenye barabara inayoelekea Ikulu, wamevunja ulinzi na kuchukua udhibiti wa eneo hilo.
Waandamanaji hao walikusanyika awali katika Uwanja wa Uhuru kabla ya kusukuma na kuvuka vizuizi vya usalama vilivyowekwa kando ya Barabara ya State House wakijaribu kusonga mbele kuelekea makazi ya Rais yanayolindwa kwa ulinzi mkali.
Waandamanaji hao, waliomobilishwa kupitia mitandao ya kijamii, walikuwa wameapa kufika Ikulu kama sehemu ya kumbukumbu ya Juni 25 ya maandamano hatari ya kupinga serikali yaliyofanyika mwaka jana.
Kikosi kikubwa cha polisi wa kukabiliana na ghasia kimepelekwa karibu na Ikulu, eneo linalolindwa ambalo haliwezi kufikiwa bila idhini rasmi kwa mujibu wa sheria.
Hii ni mara ya kwanza kwa waandamanaji kufanikiwa kuandamana katika Barabara ya State House. Mwaka 2024, waandamanaji walivamia eneo la Bunge katika hali ya mvutano kama hiyo.
Siku ya Jumanne, polisi walitoa onyo kali dhidi ya jaribio lolote la kuingia katika maeneo yanayolindwa wakati wa maandamano.
Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja aliwakumbusha wananchi kuwa ingawa Katiba inatoa haki ya kuandamana, hatua hiyo ni lazima ifanyike kwa mujibu wa sheria na kwa amani.
“Wakenya wana haki ya kuandamana, lakini hili ni lazima lifanyike katika maeneo ya umma. Kinyume cha hayo ni mkusanyiko usio halali na unaoashiria fujo,” alisema Kanja.
“Huduma ya Polisi ya Taifa itaendelea kuzuia kwa mujibu wa sheria na kwa uthabiti ukiukaji wowote wa amani unaofanywa na mtu binafsi au vikundi vinavyotenda kinyume na sheria. Aidha, watu wasiokuwa na idhini wanapaswa kuepuka kuingia katika maeneo yanayolindwa kwa mujibu wa Sheria ya Maeneo Yanayolindwa (Sura ya 204, Sheria za Kenya).”
Aliwahimiza raia pia kujiepusha na kuchokoza maafisa wa polisi wanapotekeleza majukumu yao.
Maandamano haya yanafanyika kuadhimisha kumbukumbu ya mwaka mmoja tangu maandamano ya Juni 25, 2024, ambapo takriban waandamanaji 60 waliuawa.
Waandamanaji wa kizazi cha Gen Z wanasema wanaendelea kupaza sauti dhidi ya ushuru wa kikatili, ufisadi, utawala mbovu, na ukosefu wa ufadhili kwa vyuo vikuu.
Waziri wa zamani wa Usalama wa Ndani, Dkt. Fred Matiang’i, ametangaza kwa kauli kali kuunga mkono haki za waandamanaji, akizihimiza taasisi za usalama kuwa na kiasi na akionya kuwa matumizi ya nguvu yatazidisha mgogoro.