logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Gachagua: Jamii ya Wakikuyu Yajutia Kutomsikiliza Uhuru Kuhusu Ruto

Gachagua alidai kuwa Rais Ruto amegeuka dhidi ya jamii iliyompigia kura kwa wingi wakati wa uchaguzi wa Agosti 9, 2022.

image
na Tony Mballa

Habari09 July 2025 - 14:06

Muhtasari


  • Alisema si sahihi kwa Ruto kupendekeza kuwa jamii ya Wakikuyu inaungana kumpinga, ilhali hawakuwahi kufanya hivyo kwa marais wa zamani Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta ambao wote walitoka katika jamii hiyo.
  • Gachagua alimkumbusha Ruto kwamba yeye ndiye aliyewapa wakati mgumu Kibaki na Uhuru wakati wa utawala wao.

Kiongozi wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) Rigathi Gachagua amesema kuwa jamii ya Wakikuyu inajutia kutokutii onyo alilowapa Rais wa zamani Uhuru Kenyatta kuhusu tabia ya Rais William Ruto.

Gachagua alidai kuwa Rais Ruto amegeuka dhidi ya jamii iliyompigia kura kwa wingi wakati wa uchaguzi wa Agosti 9, 2022.

“Leo, watu wa Kenya, hasa watu wa Mlima Kenya, wanajutia kwa dhati kutokutii ushauri wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta,” alisema Gachagua.

"Wakati wa maandamano ya Saba Saba, Rais Ruto alipanga genge la kihalifu lililofadhiliwa na serikali, kwa ushirikiano na polisi, ili kuua na kuharibu mali, akijaribu kuwalaumu Wakikuyu."

Alidai kuwa Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi (NIS) imenunua magari aina ya Subaru ili kutoa taswira kwamba genge la wauaji ni sehemu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI).

“Kikosi cha wauaji, kilichojifanya kuwa maafisa wa DCI, kikifanya kazi chini ya Noordin Haji, kilikuwa kimejihami kwa bunduki za kivita na kilisafiri kwa msafara wa magari ya Subaru yasiyo na alama, kikifyatua risasi na kuua waandamanaji wasio na hatia kiholela mitaani na kwenye mitaa ya makazi,” alisema.

Gachagua aliwapongeza Wakenya kutoka tabaka mbalimbali waliolaani vikali ubaguzi wa kikabila dhidi ya jamii ya Wakikuyu unaotekelezwa na serikali ya Ruto.

“Nawashukuru watu wa Kenya kwa kusimama tena dhidi ya ubaguzi huu wa kikabila dhidi ya Wakikuyu. Wakenya jana walifanya jambo la kipekee kwa kusema kuwa Wakikuyu hawafai kubaguliwa,” alisema.

Alisema si sahihi kwa Ruto kupendekeza kuwa jamii ya Wakikuyu inaungana kumpinga, ilhali hawakuwahi kufanya hivyo kwa marais wa zamani Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta ambao wote walitoka katika jamii hiyo.

Gachagua alimkumbusha Ruto kwamba yeye ndiye aliyewapa wakati mgumu Kibaki na Uhuru wakati wa utawala wao.

“Na tunataka pia kukukumbusha kuwa Mwai Kibaki alipata wakati mgumu kutoka kwako, William Ruto. Video zipo kila mahali. Huwezi kusema kuwa Mwai Kibaki hakukumbana na upinzani. Iko kwenye rekodi kuwa ulimtesa Rais Kenyatta kwa miaka mitano,” alisema Gachagua.

“Hivyo basi, ni unafiki kudai kuwa Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta walikuwa na wakati mwepesi. Shida nyingi ambazo Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta walikumbana nazo zilitoka kwako, na hii iko kwenye rekodi,” aliongeza.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved