•Njonjo ambaye alitambulika kama 'The Duke of Kabeteshire' amefariki akiwa na umri wa miaka 101.
Aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa kwanza baada ya Kenya kupata uhuru, Charles Mugane Njonjo amefariki dunia.
Waziri huyo wa zamani wa Sheria na masuala ya Katiba aliaga mwendo wa saa kumi na moja akiwa nyumbani kwake Muthaiga, Nairobi.
Njonjo ambaye alitambulika sana kama 'The Duke of Kabeteshire' amefariki akiwa na umri wa miaka 101.
Alipokuwa anathibitisha hayo, rais Uhuru Kenyatta amesema kifo cha Njonjo ni pigo kubwa kwa familia, marafiki, Kenya na Afrika yote kwa jumla.
Rais amemsherehekea marehemu kwa jukumu kubwa alilocheza katika ujenzi wa taifa na kwa kazi nzuri aliyofanya kwa kujitolea alipofanywa mwanasheria mkuu wa kwanza baada ya nchi kupata uhuru.
"Kenya inafaa kumshukuru Mhe. Njonjo kwa utawala unaoendelea wa kikatiba na kisheria kwa kazi yake nzuri alipohudumu kama Mwanasheria Mkuu wa kwanza wa nchi baada ya uhuru kati ya 1963 na 1979, na kama Waziri wa Masuala ya Katiba kati ya 1980 na 1983. Kwa niaba ya taifa la Kenya, familia yangu na kwa niaba yangu binafsi, natuma salamu za rambirambi kwa familia, marafiki na jamaa wa Mhe. Njonjo, na Wakenya wote." Rais amesema.
Rais ametakia familia ya Njonjo na Wakenya wote kwa jumla neema na ujasiri wa kupambana na majonzi ya kupoteza shujaa huyo wa taifa.
"Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Mhe. Charles Mugane Njonjo kwa amani ya milele." Amesema rais Kenyatta.