Rais Samia: 'Nimewashinda marais wanaume'

Muhtasari

•Rais Samia Suluhu anasema katika baadhi ya maeneo kwenye majukumu yake ya urais amesimamia vyema zaidi kuliko marais wengine wanaume waliomtangulia

Image: BBC

Rais wa Tanzania Samia Suluhu anasema katika baadhi ya maeneo kwenye majukumu yake ya urais amesimamia vyema zaidi kuliko marais wengine wanaume waliomtangulia.Rais wa Tanzania alisema alikabiliwa na changamoto za kutoaminiwa katika siku zake za kwanza ofisini kwa sababu yeye ni mwanamke - jambo ambalo alilazimika kulishinda.

Bi Samia alikuwa akizungumza kwenye kongamano katika mji mkuu wa Ghana Accra – ikiwa ni ziara yake ya kwanza Afrika Magharibi tangu aapishwe kuwa rais kufuatia kifo cha mtangulizi wake John Magufuli Machi 2021.“Ilikuwa vigumu sana kuwafanya watu wa Tanzania kuniamini.

Kwamba naweza kuendesha nchi sawa na wanaume – hiyo ndiyo ilikuwa changamoto kubwa,” alisema wakati wa kikao kilichoandaliwa kama sehemu ya mkutano wa kila mwaka wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB)."Katika kipindi cha mwaka mmoja nimeonyesha nguvu za wanawake, niliongoza nchi kama wanaume walivyofanya na katika mazingira mengine kwa ubora kuliko wao," aliongeza.

Kiongozi huyo wa Tanzania aliliambia jukwaa la AfDB kwamba ukuaji wa uchumi wa nchi umeshuka kutoka 6.4% hadi 4% wakati wa janga la Covid - lakini chini ya uongozi wake ulipanda hadi 5.2% na ilitabiriwa kufikia 6.7% ifikapo 2025.Kongamano hilo lililofanyika mjini Accra pia lilihudhuriwa na Rais wa Ghana Nana Akufo-Addo, Rais wa Msumbiji Filipe Nyusi na Rais wa Comoro Azali Assoumani.