Kulingana na Kituo Huru cha Kifini cha Utafiti wa Nishati na Hewa Safi (CREA), Urusi ilipata takriban dola bilioni 100 kutokana na biashara ya mafuta na gesi katika siku 100 za kwanza za vita.
Hayo yamesemwa katika ripoti mpya iliyotolewa na kituo hicho.
Ripoti ya kituo hicho ilisema bado kuna "mashimo" mengi yamesalia katika EU na juhudi za Marekani kupunguza uagizaji kutoka Urusi.
EU ilikuwa imepanga kwamba vikwazo vya mafuta kwa Urusi vingekuwa na athari kubwa, lakini usafirishaji wa mafuta ghafi ya Urusi kwenda India umeongezeka, wakati bidhaa za mafuta iliyosafishwa nchini India zinauzwa kwa Marekani na EU.
Kulingana na utafiti huo, asilimia 61 ya mauzo ya nje ya Urusi yalikwenda kwa Jumuiya ya Ulaya, ambayo ilinunua mafuta na gesi yenye thamani ya dola bilioni 60.
Kati ya hizo, dola bilioni 12.1 zilinunuliwa na Ujerumani na dola bilioni 7.8 na Italia.
China ilikuwa muagizaji mkubwa wa mafuta na gesi ya Urusi nje ya Uropa, na tangu Februari 24, Urusi imeuza bidhaa zenye thamani ya zaidi ya dola bilioni 12 kwa Uchina.
Mwanzoni mwa Juni, Umoja wa Ulaya uliidhinisha vikwazo ambavyo viliashiria kuachana kabisa na uagizaji wa Kirusi na kupunguza matumizi ya gesi ya Kirusi kwa theluthi mbili.