DJ apigwa risasi na kufariki wakati akitangaza moja kwa moja

Juan Jumalon, anayejulikana kama DJ Johnny Walker, alipigwa risasi ndani ya studio yake ya nyumbani, polisi walisema.

Muhtasari

•Bw Jumalon alikuwa akiendeleza matangazo ya moja kwa moja kwenye Facebook mwendo wa 05:30 wakati mshukiwa alipoingia kwenye chumba cha kurekodia na kumpiga risasi.

Image: BBC

Mtangazaji wa redio nchini Ufilipino ameuawa kwa kupigwa risasi alipokuwa akitangaza moja kwa moja.

Juan Jumalon, anayejulikana kama DJ Johnny Walker, alipigwa risasi ndani ya studio yake ya nyumbani, polisi walisema.

Rais Marcos Jr amelaani mauaji yamtangazaji huyo wa redio "kwa maneno makali".

Wanahabari wanne wameuawa tangu Bw Marcos Jr aingie madarakani Juni 2022, Muungano wa Kitaifa wa Wanahabari nchini Ufilipino ulisema.

"Shambulio hilo ni la kulaaniwa zaidi kwani lilitokea nyumbani kwa Jumalon, ambayo pia ilitumika kama kituo cha redio," muungano huo ulisema.

Bw Jumalon alikuwa akiendeleza matangazo ya moja kwa moja kwenye Facebook mwendo wa 05:30 saa za eneo hilo wakati mshukiwa alipoingia kwenye chumba cha kurekodia na kumpiga risasi.

Kulingana na vyombo vya habari vya eneo hilo, vikinukuu polisi, mshukiwa aliomba ruhusa ya kuingia katika chumba cha utangazaji cha Bw Jumalon "ili kutangaza jambo muhimu hewani."

Polisi wanasema tayari wamepata picha za CCTV katika eneo hilo.

Matangazo ya Bw Jumalon kawaida hupeperushwa kwenye ukurasa wa Facebook wa 94.7 Gold Mega Calamba FM, ambao una takriban wafuasi 2,400.

Mke wa DJ huyo alimpeleka mumewe hospitali mara baada ya tukio hilo, lakini inafahamika madaktari walitangaza kuwa amefariki alipofika.

Polisi walisema hawakufahamu vitisho vyovyote vya hapo awali dhidi ya maisha yake.

Rais alichapisha kwenye mtandao wa X kwamba amewaagiza polisi kufanya "uchunguzi wa kina ili kuwafikisha wahusika haraka mahakamani."

Ufilipino ni mojawapo ya maeneo hatari zaidi duniani kwa waandishi wa habari, inasema Freedom House yenye makao yake makuu nchini Marekani.