Afisa wa zamani aliyepatikana na hatia ya mauaji ya George Floyd achomwa kisu gerezani

Mfungwa huyo mwenye umri wa miaka 47 alijeruhiwa vibaya na mfungwa mwingine.

Muhtasari

•Derek Chauvin, aliyepatikana na hatia ya mauaji ya George Floyd, amechomwa kisu katika gereza la Arizona.

•Hakuna mtu mwingine aliyeripotiwa kujeruhiwa huku Chauvin akiripotiwa kunusurika katika shambulio hilo.

Image: BBC

Afisa wa zamani wa polisi wa Minneapolis Derek Chauvin, aliyepatikana na hatia ya mauaji ya George Floyd, amechomwa kisu katika gereza la Arizona, vyombo vya habari vya Marekani vinasema.

Chanzo kimoja kiliambia shirika la habari la AP kwamba mfungwa huyo mwenye umri wa miaka 47 alijeruhiwa vibaya na mfungwa mwingine.

Gazeti la New York Times, likiwanukuu watu wawili wanaofahamu hali hiyo, pia liliripoti kwamba alishambuliwa.

Chauvin anatumikia vifungo tofauti kuhusiana na kifo cha Mmarekani huyo mwenye asili ya Kiafrika, ambacho kilisababisha maandamano makubwa dhidi ya ukatili wa polisi na ubaguzi wa rangi.

Ofisi ya Magereza ilithibitisha katika taarifa kwamba mfungwa wa gereza hilo la jiji la Tucson alichomwa kisu saa 12.30 saa za nyumbani (19:30 GMT) siku ya Ijumaa.

Gereza hilo lilisema wafanyakazi walikuwa kwenye "hatua za kuokoa maisha" ya mfungwa huyo, ambaye alipelekwa hospitalini. Jina la mfungwa halikutajwa.

Hakuna mtu mwingine aliyeripotiwa kujeruhiwa huku Chauvin akiripotiwa kunusurika katika shambulio hilo.

Mauaji ya Floydd - yaliyonaswa kwenye video ya simu ya mpita njia - yalizua ghadhabu duniani kote na wimbi la maandamano dhidi ya dhuluma za ubaguzi wa rangi na polisi kutumia nguvu kupita kiasi.

Baadaye Chauvin alipatikana na hatia ya mauaji ya Bw Floyd na kuhukumiwa kifungo cha miaka 22 jela. Alihukumiwa kifungo cha miaka 20 zaidi mnamo Julai 2022 kwa kukiuka haki za kiraia za Bw Floyd.