Ukraine yaadhimisha Krismasi Disemba 25 kwa mara ya kwanza

Ukraine imekuwa ikitumia kalenda ya jadi ya Julian, ambayo pia hutumiwa na Urusi, ambapo Krismasi huadhimishwa Januari 7.

Muhtasari
  • "Sote tunasherehekea Krismasi pamoja. Katika tarehe moja, kama familia moja kubwa, kama taifa moja, kama nchi moja iliyoungana."
Image: REUTERS

Waumini wa kanisa la Orthodox nchini Ukraine wanashehekea Krismasi leo Desemba 25 kwa mara ya kwanza mwaka huu.

Ukraine imekuwa ikitumia kalenda ya jadi ya Julian, ambayo pia hutumiwa na Urusi, ambapo Krismasi huadhimishwa Januari 7.

Katika mabadiliko hayo yanayosadikiwa kujitenga na Waorthodox wenzao wa Urusi, sasa Ukraine inaadhimisha Krismasi kulingana na kalenda ya Magharibi - au Gregorian - ambayo hutumiwa katika maisha ya kila siku.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alibadilisha sheria hiyo mwezi Julai, akisema iliwaruhusu raia wa Ukraine "kuacha utamaduni wa Urusi" wa kusherehekea Krismasi mwezi Januari.

Katika ujumbe wa Krismasi uliotolewa Jumapili jioni, Bw Zelensky alisema Waukraine wote walikuwa pamoja.

"Sote tunasherehekea Krismasi pamoja. Katika tarehe moja, kama familia moja kubwa, kama taifa moja, kama nchi moja iliyoungana."

Katika jiji kuu la Kyiv, wanandoa Lesia Shestakova, Mkatoliki, na Oleksandr Shestakov, ambaye ni Mkristo wa dhehebu la Orthodox, wanasherehekea Krismasi pamoja.

Mzozo wa Israel na Gaza: Hamas yasema watu 70 wameuawa katika shambulio la Israel

Wizara ya afya ya Gaza inayoendeshwa na Hamas imesema shambulizi la anga la Israel limeua takriban watu 70 katika kambi ya wakimbizi ya Al-Maghazi katikati mwa ukanda huo.

Msemaji alisema huenda idadi ya waliofariki ikaongezeka kutokana na idadi kubwa ya familia zinazoishi katika eneo hilo.

Jeshi la Israel limeiambia BBC kuwa linachunguza ripoti za shambulio hilo.

Haya yanajiri wakati vyombo vya habari vya Israel na Kiarabu vikisema Misri, ambayo inapakana na Ukanda wa Gaza, imetoa pendekezo jipya la kusitishwa kwa mapigano kati ya Israel na Hamas.

Makumi ya watu waliojeruhiwa walikimbizwa kutoka Maghazi hadi Hospitali ya karibu ya Al-Aqsa wakiwa na picha zinazoonyesha baadhi ya nyuso za watoto zikiwa na damu na mifuko ya miili iliyorundikana nje.

Wizara ya afya inasema nyumba tatu zilipigwa katika shambulio hilo Jumapili jioni.

Kulingana na msemaji wa wizara Ashraf al-Qudra, makazi yenye watu wengi yaliharibiwa.