Mwanamume akiri kuwaua watalii watatu waliotoweka Mexico

Jesús Gerardo alikabiliwa na mahakama kwa makosa ya utekaji nyara na atafunguliwa mashtaka ya mauaji hivi karibuni.

Muhtasari

•Ndugu wa Australia Jake na Callum Robinson na rafiki yao Mmarekani Jack Carter Rhoad walitoweka tarehe 27 Aprili karibu na Ensenada.

• Mpenzi wake Ari Gisel na mwanamume mwingine wamezuiliwa kwa kushukiwa kuhusika.

Image: BBC

Mwanamume aliyeshtakiwa kwa kutoweka kwa watalii watatu katika safari ya kuteleza kwenye mawimbi nchini Mexico alikiri kuwaua, mahakama imesikiliza ushahidi huo.

Ndugu wa Australia Jake na Callum Robinson na rafiki yao Mmarekani Jack Carter Rhoad walitoweka tarehe 27 Aprili karibu na Ensenada.

Jesús Gerardo Jumatano alikabiliwa na mahakama kwa makosa ya utekaji nyara, lakini maafisa wanasema mashtaka ya mauaji yatafunguliwa hivi karibuni.

Pia anajulikana kama "El Kekas", bado hajawasilisha ombi.

Maafisa wa jimbo la Baja California wamesema watalii hao watatu - wote wakiwa na umri wa miaka ya 30 - huenda waliuawa walipokuwa wakijaribu kuzuia wizi wa matairi ya lori lao la kubebea mizigo.

Miili yao ilipatikana ikiwa imetupwa kwenye kisima cha miamba siku sita baada ya kutoweka, kila mmoja akiwa na risasi kichwani, kulingana na mamlaka za eneo hilo. Mwili wa nne pia ulipatikana kwenye kisima hicho lakini ulikuwa hapo kwa muda mrefu na haukujumuishwa kwenye kesi hiyo, waliongeza.

Jesús ameshtakiwa kwa "kutoweka kwa lazima" na mpenzi wake Ari Gisel na mwanamume mwingine wamezuiliwa kwa kushukiwa kuhusika. Majina yao ya ukoo yamefichwa na mahakama.

Wakati wa kufikishwa mahakamani Jumatano, waendesha mashtaka walimtaja Ari - ambaye hajafunguliwa mashtaka kuhusu kutoweka kwao - kama mmoja wa mashahidi wao.

Mahakama iliambiwa kijana huyo mwenye umri wa miaka 23 aliwaambia wachunguzi kwamba Jesús alifika nyumbani kwake tarehe 28 Aprili, na kumwambia kuwa alikuwa amefanya kitu kwa watu watatu.

Alimuuliza anamaanisha nini, naye akajibu "nimewaua", kikao kiliambiwa.