Waumini wafungiwa katika msikiti na kuchomwa hadi kufa

Polisi wanasema wamemkamata mshukiwa mwenye umri wa miaka 38.

Muhtasari
  • Kisa hicho kilitokea waumini walipokuwa katika sala ya alfajiri siku ya Jumatano katika eneo la Gezawa katika jimbo la Kano.

Takriban waumini 11 wameuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya mtu mmoja kushambulia msikiti katika jimbo la Kano kaskazini mwa Nigeria, polisi wamesema.

Mwanamume mmoja anadaiwa kumwagia petroli msikiti huo na kufunga milango yake kabla ya kuuchoma moto, na kuwanasa waumini wapatao 40, walisema.

Shambulio hilo lilichochewa na mzozo wa kifamilia kuhusu kugawana urithi.

Polisi wanasema wamemkamata mshukiwa mwenye umri wa miaka 38.

Kisa hicho kilitokea waumini walipokuwa katika sala ya alfajiri siku ya Jumatano katika eneo la Gezawa katika jimbo la Kano.

Wakaazi walisema moto uliteketeza msikiti huo baada ya shambulio hilo huku waumini wakisikika wakipiga mayowe walipokuwa wakihangaika kufungua milango iliyofungwa.

Baada ya kusikia mlipuko huo, majirani walikimbia kusaidia waumini waliokuwa wamenaswa, vyombo vya habari vya eneo hilo viliripoti.

Vikosi vya uokoaji vikiwemo wataalamu wa mabomu kutoka Kano vilitumwa mara moja kujibu shambulio hilo, taarifa ya polisi ilisema.

Polisi baadaye walithibitisha kuwa bomu halikutumika katika shambulio hilo.

Kikosi cha Zimamoto jimboni Kano kilisema kuwa hawakuarifiwa mapema moto huo ulipoanza, na kuongeza kuwa wangeweza kudhibiti hali hiyo haraka zaidi.