Miili yote yapatikana baada ya watu 62 kufariki katika ajali ya ndege

Timu zilikuwa zikifanya kazi kutafuta na kutambua waathirika wa janga hilo.

Muhtasari

•Ndege ilianguka katika jimbo la São Paulo, Brazil na kusababisha vifo vya watu wote waliokuwa ndani ya ndege hiyo.

Image: BBC

Miili yote imepatikana katika eneo la ajali ya ndege katika jimbo la São Paulo nchini Brazil na kusababisha vifo vya watu wote waliokuwa ndani ya ndege hiyo, mamlaka imethibitisha.

Timu zilikuwa zikifanya kazi kutafuta na kutambua waathirika wa janga hilo baada ya turboprop ya injini-mbili inayoendeshwa na shirika la ndege la Voepass kushuka katika mji wa Vinhedo.

Idadi ya walioangamia mpaka Jumamosi ilikuwa imefika 62.

Voepass lilisema hapo awali kwamba ATR 72-500 ilikuwa na abiria 57 na wafanyakazi wanne kati ya Cascavel katika jimbo la kusini la Paraná hadi uwanja wa ndege wa Guarulhos katika jiji la São Paulo. Lakini baadaye ilithibitisha kuwa kulikuwa na abiria mwingine ambaye hajulikani alipo kwenye ndege hiyo.

Picha zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii zilionesha ndege ikishuka wima, ikizunguka huku ikianguka.

Jimbo la São Paulo lilisema lilihitimisha operesheni yake ya kuondoa miili ya waathirwa kutoka eneo hilo saa 18:30 saa za ndani (22:30 BST) siku ya Jumamosi.

Iliongeza kuwa miili hiyo, wanaume 34 na wanawake 28, walikuwa wakihamishiwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti cha polisi katika mji wa São Paulo, ambapo watatambuliwa na kukabidhiwa kwa familia.

Wawili kati ya waathiriwa, nahodha na afisa mkuu, tayari wametambuliwa, serikali ilithibitisha.

Hapo awali, Capt Maycon Cristo, msemaji wa idara ya zima moto, alisema timu zinategemea mambo kadhaa kusaidia kutambua abiria.

Hizi ni pamoja na hati na nafasi zao walizokuwa wameketi, pamoja na simu za mkononi zilizopatikana kutoka kwa baadhi ya walioathirika.