logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Zambia: Polisi Wakamata Waganga 2 Kwa Kupanga Njama Ya Kumroga Rais Hakainde

Washukiwa hao wawili wanakabiliwa na mashtaka ya kufanya uchawi, kumiliki hirizi na ukatili kwa wanyama.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Kimataifa21 December 2024 - 07:27

Muhtasari


  • Jasten Mabulesse Candunde, 42, na Leonard Phiri, 43, wanadaiwa kukodiwa na Nelson Banda, mdogo wa mbunge mtoro Jay Banda, ili kumroga rais.
  • Jay Banda alitoroka kutoka mikononi mwa polisi Agosti 2024 akikabiliwa na shtaka la wizi wa kupindukia. Mahali alipo hajulikani.
  • Washukiwa hao wawili wanakabiliwa na mashtaka ya kufanya uchawi, kumiliki hirizi na ukatili kwa wanyama.

WATU wawili wamekamatwa kwa madai ya kupanga njama ya kumdhuru Rais wa Zambia Hakainde Hichilema kwa kutumia uchawi, polisi walisema Ijumaa.


Msemaji wa polisi, Rae Hamoonga alisema katika taarifa yake kwamba washukiwa hao wawili, Jasten Mabulesse Candunde, 42, na Leonard Phiri, 43, wanadaiwa kukodiwa na Nelson Banda, mdogo wa mbunge mtoro Jay Banda, ili kumroga rais.


Jay Banda alitoroka kutoka mikononi mwa polisi Agosti 2024 akikabiliwa na shtaka la wizi wa kupindukia. Mahali alipo hajulikani.


Washukiwa hao wawili wanakabiliwa na mashtaka ya kufanya uchawi, kumiliki hirizi na ukatili kwa wanyama.


"Washukiwa hao walikutwa na hirizi za aina mbalimbali, akiwemo kinyonga aliye hai, na wanadaiwa kuwa waganga," Hammonga alisema, na kuongeza kuwa dhamira yao "ilikuwa ni kutumia hirizi kumdhuru Mkuu wa Nchi, Mheshimiwa Rais Hakainde Hichilema.”


Msemaji wa polisi alisema washukiwa hao walifichua kwamba walikubali kupokea malipo kamili ya $7,400.


"Dhamira yao iliyodaiwa ilikuwa kutumia hirizi kudhuru" Rais Hakainde Hichilema, alisema taarifa ya polisi, iliyotolewa Ijumaa.


Watu wengi katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika wanaamini - na wanaishi kwa hofu ya - uchawi.


Polisi walisema Bw Candunde na Bw Phiri waliajiriwa na Nelson Banda, nduguye mdogo wa Mbunge Emmanuel “Jay Jay” Banda.


Mbunge huyo aliripotiwa kukamatwa mwezi uliopita katika nchi jirani ya Zimbabwe kutokana na mashtaka ya wizi, ambayo anayakanusha, lakini hajaonekana hadharani.


Pia anadaiwa kutoroka kutoka kizuizini mwezi Agosti alipokuwa akisubiri kufikishwa mahakamani.


Chama cha upinzani cha Patriotic Front (PF), kinachoongozwa na Rais wa zamani Edgar Lungu, hapo awali kilidai kuwa mashtaka haya yanachochewa kisiasa.


Emmanuel Banda, ambaye amekuwa mbunge huru tangu 2021, awali alihusishwa na Lungu, ambaye alipoteza urais na Hichilema mwaka huo.


Katika taarifa yao, polisi walisema kwamba mdogo wa mbunge huyo, Nelson, "kwa sasa yuko mbioni".


Bw Candunde na Bw Phiri wameshtakiwa chini ya Sheria ya Uchawi ya Zambia kwa "kumiliki hirizi", "kudai ujuzi wa uchawi" na "ukatili kwa wanyama pori".


Wawili hao walipatikana na "hirizi mbalimbali", akiwemo kinyonga aliye hai, polisi waliongeza.


Washukiwa hao wanazuiliwa na watafikishwa mahakamani "hivi karibuni", polisi walisema, lakini hawakutoa tarehe kamili ya kusikilizwa kwa kesi hiyo. Bado hawajazungumza hadharani kuhusu tuhuma hizo.


 



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved