Dereva wa matatu afungwa miaka 3 kwa kusababisha kifo cha mpita njia

Patrick Magu alipewa faini mbadala ya Shilingi laki 200,000 akishindwa atatumikia kifungo cha miaka mitatu.

Muhtasari

• Hakimu Esther Kimilu pia amesimamisha leseni yake ya udereva kwa muda wa mwaka mmoja.

• Magu alidaiwa kuendesha basi dogo aina ya Isuzu lenye nambari za usajili KBR 065B kwa mwendo wa kasi na hatari kwa umma.

 

Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Edward Mbugua katika kituo cha polisi cha Kigumo Jumanne. Picha: Alice Waithera
Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Edward Mbugua katika kituo cha polisi cha Kigumo Jumanne. Picha: Alice Waithera

Dereva wa matatu amehukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela baada ya kupatikana na hatia ya kusababisha kifo cha bintiye Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Edward Mbugua.

Patrick Magu alipewa faini mbadala ya Shilingi laki 200,000 akishindwa atatumikia kifungo cha miaka mitatu.

Magu alishtakiwa kwa kusababisha kifo cha Meline Waithera Mbugua mnamo Juni 17 mwaka 2021.

Hakimu Esther Kimilu pia amesimamisha leseni yake ya udereva kwa muda wa mwaka mmoja.

Katika uamuzi wake, Hakimu alibainisha kuwa katika mahojiano yake Magu alijuta na alikiri kwamba ni kweli aligeuza gari hilo bila uangalifu.

Wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo, mahakama ilisikia kuwa Magu aligeuza gari hilo bila kujali watumiaji wengine wa barabara, hali iliyopelekea marehemu kuwa katikati ya magari mawili.

Mahakama pia ilizingatia kuwa gari alilokuwa akiendesha Magu halifai kuwa barabarani na kwamba baada ya kusababisha ajali hiyo alijisalimisha kwa polisi.

Mahakama ilisikiza kwamba Waithera aligongwa na kisha kuingizwa kwenye gari lingine, na kusababisha kifo chake kando ya barabara ya Tom Mboya jijini Nairobi mnamo Juni 17 mwaka jana.

Magu alidaiwa kuendesha basi dogo aina ya Isuzu lenye nambari za usajili KBR 065B kwa mwendo wa kasi na hatari kwa umma.