Kijana afungwa siku 14 jela kwa kuiba nyama ya kuku yenye thamani ya Ksh 300

Hukumu huu uliafikiwa baada ya kijana huyo mwenye umri wa miaka 21 kushindwa kulipa faini ya Ksh 1000.

Muhtasari

• Kijana huyo alisema kuwa alifanya kitendo hicho kutokana na njaa na kutaka mahakama impe msamaha ila akashindwa kulipa faini na hivyo kulazimika kuhudumia kifungo hicho.

Mfungwa akiwa jela
Mfungwa akiwa jela
Image: Mfungwa Jela

Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 21 amehukumiwa kifungo cha siku 14 jela kwa kukiri kosa la kuiba nyama ya kuku yenye thamani ya shilingi 300.

Kijana huyo atalazimika kuhudumia kifungo hicho baada ya kushindwa kulipa faini ya shilingi 1000.

Mwanaume huyo aliripotiwa kuiba kuku huyo katika eneo la Kayole jijini Nairobi. Bw Mwai alikiri kwamba aliiba kuku wa mwajiri wake – Quality Meat Packers mnamo Novemba 16, 2022.

Bw Martin Mwai alipewa adhabu hiyo na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mercy Thibaru wa Mahakama ya Sheria ya Makadara baada ya kukiri mashtaka ya wizi.

 Tajiri mwenye kampuni hiyo ya kuuza nyama ya kuku alisema kuwa alipigiwa simu ya mlinzi wa lango kuwa wamemkamata kijana huyo akijaribu kuondoka na nyama ya kilo yenye uzito wa kilo moja ambayo alikuwa ameficha ndani ya suruali yake.

Mtuhumiwa alisindikizwa hadi Kituo cha Polisi cha Mawe Mbili akiwa na nyama hiyo. Nyama hiyo ilipigwa picha na kurejeshwa kwa Bw Munyaka ambaye ni mwenye kampuni hiyo nhuku Bw Mwai akiwekwa kizuizini kabla ya kuachiliwa kwa dhamana ya Sh5000.

Bw Mwai aliambia mahakama kwamba aliiba kwa sababu alikuwa na njaa. Aliomba msamaha.

Hii si kesi ya kwanza ya ajabu kuripotiwa nchini Kenya kwani miezi kadhaa iliyopita kijana mwingine kwa jina Alvin Chivondo alikamatwa kwa kuiba bidhaa katika duka la jumla la Naivas jijini Nairobi.

Kesi hiyo iligonga vichwa vya habari baada ya kuhukumiwa, kuwafanya watu mbalimbali kujitokeza ili kumlipia fidia ya faini kijana huyo ambapo pia Mike Sonko aliarifiwa kumpa kazi katika moja ya ofisi zake jijini.