Mwanamke wa miaka 23 aliyeripotiwa kufumaniwa kitandani akiwa na mvulana wa miaka 16 katika mtaa wa Embakasi jijini Nairobi amepandishwa kizimbani kwa kosa la unajisi.
Mwanamke huyo aliyetambulika kwa jina Damaris Kerubo alisemekana kumfanyia kijana huyo unajisi kati ya mwezi Aprili hadi Julai mwaka huu.
Upande wa mashtaka uliambia mahakama kwamba Kerubo alifumaniwa katika kitanda cha mvulana huyo ndani ya nyumba ya wazazi wake.
Jirani aliyeripotiwa kumfumania alikuwa amekwenda kuchukua ufunguo alipomfumania kwenye kitendo cha mvulana huyo chini ya umri wa miaka 18.
Katika mkondo wa pili, jirani huyo huyo alimfumania tena Kerubo akiwa na mvulana huyo ndani ya nyumba yake sasa, na hapo ndipo aliamua kumripoti kwa wazazi wake.
Mvulana huyo hata hivyo alikana kunajisiwa alipohojiwa na mama yake.
Kijana huyo ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili baadae alimsimulia ndugu yake kisa hicho na kumtaka kumuombea radhi kwa mama yake, kwani awali alikuwa amekana mbele ya mamake.
Katika mkondo wa tatu, jirani tena alimambia mama wa mvulana huyo kwamba alimfumania Kerubo tena na mwanawe na hapo ndipo waliamua kuchukua hatua ya kupiga ripoti kwa vyombo vya sheria.
Hata hivyo, mvulana huyo ambaye pia alitiwa nguvuni na polisi alisema ni yeye aliyemtongoza Kerubo na akakubali kuwa mpenzi wake tangu Aprili.
Mvulana huyo alisema kwamba Kerubo alikuwa mteja wa kila siku katika kibanda cha mboga cha mamake na hapo ndipo alimkuta na kumtongoza na akakubali.
Kerubo alikanusha mashtaka mbele ya hakimu mkaazi wa mahakama ya Makadara na kuachiliwa kwa dhamana ya shilingi laki mbili au mdhamana wa kiasi sawa.
Kesi hiyo tena itatajwa Agosti 15 na hukumu kutolewa Septemba 28.