Ruto azungumzia video yake akitimka mbio kwa miguu siku ya mwisho ya kampeni

Rais alisema kwamba alikuwa anajua Raila angemshinda kura Kiambu na ndio maana aliona kama lazima kufunga kwa maombi katika uwanja wa Kirigiti, Kiambu.

Muhtasari

• Ilikuwa ni dharura kwamba tufanye jambo na mkutano huo ukaonekana kama wa kutokosa. Na tulifika hapo dakika 18 hadi saa kumi na mbili jioni - Ruto.

• Alisema kuwa kutokana na kufika pale zikisalia dakika chache kwa makataa ya IEBC, maombi yao yalifanya miujiza na kushinda kura.

Ruto azungumzia video yake akikimbia kwa mguu
Ruto azungumzia video yake akikimbia kwa mguu
Image: Facebook

Kwa mara ya kwanza rais William Ruto amefichua ni kwa nini alionekana kweney video akikimbia ili kufikia helkopta iliyokuwa inafaa kumsafirisha hadi kaunti ya Kiambu baada ya kumalizika kwa mkutano mkuu wa Kenya Kwanza katika uwanja wa Nyayo Nairobi, siku ya mwisho ya kufanya kampeni kuelekea uchaguzi mkuu uliopita wa Agosti 9.

IEBC ilikuwa imeratibu Agosti 6 kuwa siku ya mwisho kufanyika kwa kampeni za hadharani, siku tatu tu kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa Agosti 9.

Ruto na wafuasi wa Kenya Kwanza walijumuika katika uwanja wa Nyayo jijini Nairobi kwa mkutano wa mwisho kufunga kampeni huku wapinzani wao wakikongamana uwanja wa Kasarani sambamba.

Baada ya kumalizika kwa siku hiyo, mwendo wa jioni Ruto alionekana akitimka mbio kuelekea uwanja wa Wilson ambapo alitarajia kupata ndege ya kumsafirisha hadi kaunti ya Kiambu uwanja wa Kirigiti kwa mkutano wa mwisho kabisa kufunga hiyo siku, video ambayo ilisambazwa pakubwa mitandaoni.

 Jumapili katika ibada ya kanisa moja eneo la Lang’ata, rais Ruto alifunguka kuhusu video ile ikimuonesha akikimbia na kusema kwamba alikuwa alikuwa na msukumo fulani kutoka ndani mwake ulimtuma kuwa sharti angefunga kipindi cha kampeni kwa maombi katika uwanja huo.

“Tulishughulikia mikutano hiyo yote na bado tulikuwa na tatizo moja lililokuwa likitushtua katika Kaunti ya Kiambu ... Muda ulikuwa ukienda sana na tuligawanyika kati ya kuhudhuria mkutano wa kufunga katika uwanja wa Kirigiti ... Tulikuwa na chini ya dakika 30 kufanya hivyo,” Ruto alisema.

Rais alisema kuwa hakuwa na Imani ya kushinda uchauzi huo dhidi ya Raila Odinga ambaye alikuwa mpinzani wa moto haswa baada ya kuungwa mkono na rais aliyekuwa ameshikilia dola kipindi hicho, Uhuru Kenyatta.

"Dalili zote kulingana na kura za maoni, na vyombo vya habari vilitoa dhana kwamba hatukupaswa kushinda Kiambu ... Ilikuwa ni dharura kwamba tufanye jambo na mkutano huo ukaonekana kama wa kutokosa. Na tulifika hapo dakika 18 hadi saa kumi na mbili jioni, ambao ulikuwa muda rasmi uliowekwa kwa makundi yote kufunga kampeni za umma." alisema.

Ruto alisema kuwa baada ya hotuba fupi fupi, alijua kuwa alifaa kufanya kitu kingine ambapo aliwataka umati kuvua kofia zao kwa maombi.

“Maombi yanafanya kazi, kwani hatukushinda kura ya kitaifa tu bali pia tulishinda Kiambu,” Rais Ruto alisema.