Ruto afichua thamani ya KICC, aeleza kwa nini anataka kuikabidhi kwa mwekezaji wa kibinafsi

Rais alikariri kuwa serikali inatafuta mwekezaji wa kimkakati ambaye atalifanya jengo hilo kuwa la kibiashara.

Muhtasari

•Rais alidai kuwa usimamizi mbovu wa jengo hilo katika miaka ya nyuma umefanya imekuwa ngumu sana kwa serikali kupata mapato kulingana na thamani yake.

•Alisema inapaswa kuwa inaiingizia serikali takriban 10% ya thamani yake kila mwaka, jambo ambalo halijafanyika kwa miaka mingi iliyopita.

katika kikao cha wanahabari katika Ikulu ya Nairobi.
Rais William Ruto katika kikao cha wanahabari katika Ikulu ya Nairobi.
Image: REBECCA NDUKU

Rais William Ruto amefichua kuwa nia ya kubinafsisha Jumba la Mikutano  KICC ni ili kuhakikisha inatumika vyema na pesa za maana zinapatikana kutokana na jengo hilo.

Katika mahojiano na waandishi wa habari mbalimbali  siku ya Jumapili jioni, amri jeshi mkuu huyo alidai kuwa usimamizi mbovu wa jumba hilo la kitaifa katika miaka ya nyuma umefanya imekuwa ngumu sana kwa serikali kupata mapato kulingana na thamani yake.

Alisema kuwa jengo hilo refu ambalo limekuwepo kwa takriban miongo mitano iliyopita lina thamani ya shilingi  bilioni 30 na kwa mujibu wake; inapaswa kuwa inaiingizia serikali takriban 10% ya thamani yake kila mwaka, jambo ambalo halijafanyika kwa miaka mingi iliyopita.

"KICC ni jengo la kitambo; ni katikati mwa jiji. Nilipokuja Nairobi kwa mara ya kwanza, nilifika kwenye sehemu hiyo ya picha ambapo tulikuwa tumeshikilia KICC juu. Hilo litaendelea, watu wataendelea kupiga picha katika mahakama ya KICC," Rais Ruto alisema.

Kuhusu kwa nini inabinafsishwa, alieleza, "Lakini hiyo sio sababu ya KICC kujengwa, haikujengwa kwa kupiga picha. Ilijengwa kama mali ya kitaifa. KICC leo inathaminiwa kwa bilioni 30, tunapata pesa ngapi kutoka. KICC??Mwaka jana tulipata shilingi milioni 30, mwaka mwingine tulipata nadhani shilingi milioni 40. Ni upotevu gani? Kwa sababu inasimamiwa bila ufanisi."

Rais alidai kuwa kutokana na usimamizi mbovu wa KICC, hivi majuzi alilazimika kuongeza Ksh1.8bilioni wakati viongozi wa Afrika walipokutana kwa ajili ya Mkutano wa Hali ya Hewa wa Afrika.

"Ninachosema ni, badala ya kuwa na KICC kama jengo la ofisi, jengo nzima lina ofisi ya huyu na yule, hawalipi chochote), kwa nini tusiibadili KICC ili iwe International Conference Centre ambayo ilijengwa iwe tuwe tunapata shilingi bilioni 3 kwa mwaka hatupati bilioni tatu tunapata milioni 29 hii ni asset ya Kenya hii ni mali ya watu wa Kenya," alisema.

Rais alikariri kuwa serikali inatafuta mwekezaji wa kimkakati ambaye atalifanya jengo hilo kuwa la kibiashara na kuhakikisha linasimamiwa ipasavyo.