• Muswada wa Marekebisho ya katiba (BBI) umepata uungwaji mkono katika kaunti 24 ambazo zinahitajika kuupeleka kwa kura ya maoni.
Muswada wa Marekebisho ya katiba (BBI) umepata uungwaji mkono katika kaunti 24 ambazo zinahitajika kuupeleka kwa kura ya maoni.
Muswada huo maarufu kama BBI ulipelekwa kwa mabunge ya kaunti baada ya tume ya IEBC kuthibitisha zaidi ya saini milioni 3.1 za kuunga mkono.
Magavana waliongoza juhudi za kuwashawishi wakilishi wadi katika kaunti zao ili kuunga mkono Muswada huo.
Rais Uhuru Kenyatta pia aliwaahidi ruzuku ya shilingi milioni 2 kila mmoja wakilishi wadi kununua gari.
Kufikia sasa ni kaunti moja tu - Baringo, ambayo ilipiga kura kuukataa muswada huo.
Kaunti ambazo zimepitisha musuada huo kufikia sasa ni Kakamega, Narok, Makueni, Nyamira, Taita Taveta, Kitui, Bungoma, Murang’a, Machakos, Lamu, Nyeri, Nyandarua, Kirinyaga, Garissa, Mombasa, Busia, Siaya, Kajiado, Homa Bay,Trans Nzoia, Nakuru,West Pokot, Vihiga miongoni mwa kaunti zingine.
Kulingana na katiba muswada huo sasa utapelekwa kwa bunge la kitaifa na seneti na unahitaji kuidhinishwa na wabunge na maseneta kabla ya kuwasilishwa kwa rais Uhuru Kenyatta.
Ni rais atakaye amua kama atauwasilisha kwa tume ya IEBC kwa kura ya maamuzi kufanyika au kuidhinisha baadhi ya sheria ambazo hazihitaji kufanyiwa kura ya maamuzi.