Jamaa anayedaiwa kupanga mauaji ya wanaume watatu na kuchoma gari lao Kilifi atiwa mbaroni

Mshukiwa anatarajiwa kutoa majibu zaidi kuhusiana na mauaji hayo.

Muhtasari

•Robert Mganga alipatikana katika mtaa wa Tassia, Nairobi mida ya saa nne unusu siku ya Ijumaa alikokuwa amejificha baada ya kuwatoroka polisi hapo awali

•Watatu hao walikuwa wameenda kununua shamba katika kijiji cha Junju B wakati walivamiwa na kikundi cha watu waliokuwa wamejihami kwa panga.

•Miili ya watatu hao ilipatikana karibu na shule ya upili ya Junju ikiwa na alama za kukatakatwa kichwani na alama za  kuburuzwa chini mgongoni.

Image: TWITTER//DCI

Polisi wanamzuilia jamaa mmoja anayeaminika kuwa mhusika mkuu kwenye mauaji ya wanaume watatu katika kijiji cha Junju B kaunti ya Kilifi mnamo Julai 7 mwaka huu.

Robert Mganga alipatikana katika mtaa wa Tassia, Nairobi mida ya saa nne unusu siku ya Ijumaa alikokuwa amejificha baada ya kuwatoroka polisi hapo awali.

Kulingana na DCI, inaaminika kuwa Mganga ndiye alipanga njama ya kuwaua Sidik Anverali Mohammed Sidik 46, James Kazungu Kafani na dereva wao ambaye hajatambulishwa.

Watatu hao walikuwa wameenda kununua shamba katika kijiji cha Junju B wakati walivamiwa na kikundi cha watu waliokuwa wamejihami kwa panga.

Bw Kazungu ambaye alikuwa ajenti wa shamba alijaribu kuwabembeleza watu wale wasikatize maisha yao ila maombi yake yaliangulia patupu. Baada yao kuuawa kwa kukatakatwa na panga,gari lao aina ya Toyota Fielder liliteketezwa.

Miili ya watatu hao ilipatikana karibu na shule ya upili ya Junju ikiwa na alama za kukatakatwa kichwani na alama za  kuburuzwa chini mgongoni.

Mauaji hayo yaliibua maswali mengi kwa wanafamilia wa marehemu huku wengine wao wakidai kuwa yalitekelezwa na watu ambao walikuwa wanafahamiana vizuri.

 Uchunguzi wa wapelelezi wa DCI ulibaini kuwa Mganga ndiye mshukiwa mkuu wa kitendo hicho cha unyama.

Mshukiwa anatarajiwa kutoa majibu zaidi kuhusiana na mauaji hayo.