Polisi 3 washtakiwa kufuatia kutoroka kwa Masten Wanjala

Muhtasari
  • Polisi waliomba siku 14 kuwazuilia maafisa hao - Phillip Mbithi, Boniface Mutuma na Precious Mwinzi - kuwaruhusu kumaliza uchunguzi
Image: DCI

HABARI NA ANNETTE WAMBULWA;

Maafisa watatu wa polisi ambao walikuwa kazini wakati Masten Wanjala alitoroka kutoka chini ya ulinzi wa polisi Alhamisi wakifikishwa katika korti ya Milimani.

Polisi waliomba siku 14 kuwazuilia maafisa hao - Phillip Mbithi, Boniface Mutuma na Precious Mwinzi - kuwaruhusu kumaliza uchunguzi.

Katika hati ya kiapo ya Mkaguzi Mkuu Wanga Masake, serikali inasema maafisa hao watatu walikamatwa mnamo Oktoba 13 kwa tuhuma za kutenda kosa la kumsaidia mfungwa kutoroka kinyume na Kifungu cha 124 cha Kanuni za Adhabu.

Masake alisema watatu hao walidaiwa kupuuza kuzuia kutoroka kwa Wanjala - jukumu ambalo walilazimika kutekeleza chini ya Sheria ya Huduma ya Polisi ya Kitaifa.

"Kosa lilitokea usiku wa Oktoba 12 na 13 na mtuhumiwa hajakamatwa tena," inasema.

Alisema uchunguzi wa awali unafichua watatu walizembea na kumsaidia mtuhumiwa kutoroka kutoka kizuizini.

Mwanasheria Danstan Omari, akiwakilisha polisi hao 3, alisema atapinga maombi ya kuwazuia wateja wake.