• Wezi hao walivamia chumba cha kuhifadhi maiti cha Yatta iliyoko kaunti ya Machakos na kufanya uharibifu.
• Inaripotiwa kuwa genge hilo lilikuwa limelipwa kutekeleza ubinadamu huo.
Jamaa mmoja mwenye umri wa miaka 30 ametiwa mbaroni na polisi kwa madai ya kuvamia chumba cha kuhifadhi maiti cha Yatta akiwa na wenzake siku ya Jumapili.
Mshukiwa mkuu ni mtoto wa mumiliki wa shamba ambamo makafani hiyo imejengwa.
Kulingana na Kamanda wa polisi wa Yatta, Bernard Rono genge hilo liliigia ndani ya makafani na kuwadunga kisu maiti kabla kuharibu gari la kubebea maiti.
Mmiliki wa makafani hiyo Gideon Mule ambaye alishtushwa na kitendo hicho alimshutumu mwenye ardhi hiyo kwa kutotii agizo la mahakama kulipa shilingi milioni 7.
Mule alisema kuwa mwenye shamba alikuwa amekodi majambazi hao na kuwataka wamfurushe kabla hajafidiwa.
"Anataka niondoke, ilhali mahakama ilieleza kwa kinaga ubaga kuwa anilipe shilingi milioni 7 ndio nihame. sasa amefanya vitisho na mashambulizi," Bwana Mule alisema.
Mule aliongeza kuwa genge hilo liliharibu magari ya kubebea maiti, huku maiti moja ikiharibiwa kabisa.
“Vioo vya magari ya kubebea maiti vilivunjwa na mwili mmoja uliharibiwa kabisa hata familia ya marehemu inahangaika,” Mule alisema.