Jumwa ataka askari anayeshutumiwa kwa kumnajisi mtoto kukamatwa

Waziri huyo alisema afisa wa polisi kama huyo anaendeleza unyanyasaji wa kingono na kijinsia.

Muhtasari
  • Haya yanajiri baada ya naibu kamanda wa polisi wa Kilifi Wily Simba kusema afisa huyo wa polisi ametoweka baada ya kisa hicho
Image: FACEBOOK// AISHA JUMWA

Waziri wa Jinsia Aisha Jumwa ametoa agizo la kukamatwa kwa afisa wa polisi anayeshtakiwa kwa kunajisi mtoto mdogo.

Jumwa anataka kikosi cha usalama cha Kilifi kumkamata na kumfungulia mashtaka afisa huyo anayedaiwa kumnajisi msichana mwenye umri wa miaka 15 kutoka kijiji cha Marereni eneo bunge la Magarini, Kilifi.

Waziri huyo alisema afisa wa polisi kutoka kituo cha polisi cha Marereni alimnajisi msichana huyo katika nyumba ya kulala wageni iliyo karibu, msichana huyo alipokuwa akirejea nyumbani baada ya kutoka kazini mnamo Novemba 4 mwendo wa saa tisa jioni.

“Fikiria mtu amebakwa na maafisa wa polisi hawakuweza kuchukua hatua. Inashangaza kwamba naibu kamanda wa kaunti anaweza kusimama hapa na kusema kwamba mshukiwa alitoroka,” alisema.

Jumwa alikuwa akizungumza katika uwanja wa Water ground katika mji wa Kilifi wakati wa uzinduzi wa kitaifa wa siku 16 za kupinga unyanyasaji wa kijinsia.

Waziri huyo alisema afisa wa polisi kama huyo anaendeleza unyanyasaji wa kingono na kijinsia.

Haya yanajiri baada ya naibu kamanda wa polisi wa Kilifi Wily Simba kusema afisa huyo wa polisi ametoweka baada ya kisa hicho.

Jumwa alisema ikiwa mshukiwa hatakamatwa basi naibu kamanda wa kaunti na Waziri wa Usalama wa Ndani Kithure Kindiki watajibu.

"Siwezi kustahimili tabia isiyopendeza katika kaunti yangu, ilhali mimi ni Waziri wa Jinsia," alisema.

Waziri huyo alisema ukatili wa kijinsia hugharimu nchi Sh46 bilioni kila mwaka, huku kaunti za Kilifi, Samburu na Bungoma zikiongoza mtawalia.