Hatimaye DCI watoa ripoti kuhusu kifo cha utata Jeff Mwathi

Awamu ya kwanza imekamilika na awamu ya pili itajumuisha kuhojiwa kwa watu waliotajwa kuwa wenye maslahi katika kifo cha Jeff.

Muhtasari

• Awamu ya kwanza ilijumuisha kuhojiwa kwa mashahidi na pia kuchambuliwa kwa kina kwa mkanda wa CCTV.

Jeff Mwathi, aliyefariki kwa utata nyumbani kwa DJ Fatxo
Jeff Mwathi, aliyefariki kwa utata nyumbani kwa DJ Fatxo
Image: Facebook//Simon Mwangi Muthiora

Hatimaye wapelelezi wa jinai DCI, kitengo cha kuchunguza visa vya mauaji ya kinyumbani wametoa taarifa iliyokuwa imesubiriwa kwa hamu kuu na Wakenya kufuatia kifo chenye utata cha kijana Jeff Mwathi aliyefariki nyumbani kwa DJ Fatxo wiki chache zilizopita.

DCI walijivika njuga kuzamia uchunguzi wa kifo cha kijana huyo baada ya malalamishi mengi kutoka kwa Wakenya ambao walionesha kutoridhishwa kwao na jinsi maafisa wa usalama kutoka kituo cha polisi cha Kasarani walivyokuwa wakiendesha uchunguzi huo.

DCI Ijumaa wiki jana walitangaza kuanzisha uchunguzi dhidi ya kifo cha Jeff, ambaye sehemu ya watu mitandaoni wanahisi huenda alikuwa mwathiriwa wa visa vya ushoga na wengine waksiema kuwa alijiua kwa kujitupa kutoka ghorofa ya 10, katika chumba cha DJ Fatxo mtaani Kasarani.

“Idara ya Upelelezi wa Upelelezi wa Mauaji ya Jinai inayochunguza kifo cha Geoffrey Mwathi Ngugi almaarufu Jeff kilichotokea Februari 22, 2023 wamekamilisha awamu ya kwanza ya uchunguzi wao,” sehemu ya taarifa ya DCI ilisoma.

Mchakato huo ulijumuisha mahojiano ya kundi la kwanza la mashahidi katika kesi hiyo, uchunguzi wa kimahakama wa eneo la tukio na kupatikana kwa picha za CCTV zilizonasa dakika za mwisho za marehemu.

Wataalamu wengine kadhaa wa Uchunguzi wa kina walio katika Maabara ya Kitaifa ya Upelelezi ya DCI ambao wanajumuisha timu ya kushughulikia Mauaji wamekusanya kwa usawa ushahidi muhimu na huo unachambuliwa kisayansi.

“Sasa tunaendelea na awamu ya pili ya upelelezi ambapo watu kadhaa wenye maslahi katika kesi hiyo watahojiwa na mapendekezo yanayofaa kutolewa kabla ya kupelekwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ili kuchukuliwa hatua. Wakati huo huo, umma unaombwa kuwa na subira wakati DCI inapojaribu kubainisha hali zinazozunguka kifo cha ghafla cha Jeff,” ripoti ilisoma.