Msiwalazimishe Wakenya kutoa ushuru wa nyumba-Raila Kwa Ruto

Mbunge huyo alieleza kuwa makato ya Hazina ya Nyumba sio kodi bali ni mpango wa kuweka akiba.

Muhtasari
  • “Anachosema Rais ni kwamba ukishaona hutaki kuchangia zaidi baada ya miaka saba, una mkakati wa kutoka,
Ruto aapa kuendelea kumuita Odinga "my brother" ili kumaliza maandamano
Ruto aapa kuendelea kumuita Odinga "my brother" ili kumaliza maandamano
Image: Facebook

Kiongozi wa Azimio la Umoja Raila Odinga ameikashifu serikali kuhusu pendekezo la lazima la Ushuru wa Makazi wa asilimia 3.

Akihutubia wanahabari Jumanne, Raila alisema hakuna Mkenya anayepaswa kulazimishwa kuwekeza, bali awe na chaguo kuhusu kile anachotaka kuchangia.

“Nikitaka kuwekeza lazima niwe na chaguo, nisilazimishwe kuwekeza, lazima mniulize nataka kuwekeza au la, lazima kuwe na uchaguzi na mashauriano,” alisema.

Kinara huyo wa Upinzani aliongeza kuwa baadhi ya Wakenya tayari wana nyumba na hawafai kutozwa ushuru huo.

"Kwanza waulize kujua kama wako tayari kutozwa ushuru na kwa nini umtoze kodi mtu ambaye ana nyumba?" Raila aliuliza.

Mbunge wa Belgut Nelson Koech alikuwa amesema mtu anaweza kujiondoa katika kulipa ushuru huo baada ya miaka saba.

Mbunge huyo alieleza kuwa makato ya Hazina ya Nyumba sio kodi bali ni mpango wa kuweka akiba.

“Anachosema Rais ni kwamba ukishaona hutaki kuchangia zaidi baada ya miaka saba, una mkakati wa kutoka, unaweza kudai fedha zako kwa sababu ni zako. " Koech alisema.

Koech alisema mradi wa nyumba utaunda ajira mara moja na kwa kila nyumba itakayojengwa watu watano wataajiriwa.

Rais William Ruto alikuwa amewasilisha hoja ya kuwasilisha makato ya ziada ya ushuru wa nyumba katika pendekezo la Mswada wa Fedha wa 2023.

Ruto alisema wafanyikazi wanaolipwa watakatwa asilimia 3 ya mishahara yao ambayo italingana na waajiri lakini isizidi Sh5,000 ya mishahara yao kwa Hazina ya Makazi ili kusaidia mradi wa nyumba za bei nafuu.