Nyeri: Mume amgonga mkewe kichwani kwa nyundo na kumuua kabla ya kujitia kitanzi

Wanakijiji waliuona mwili wa mwanamume huyo ukiwa umening'inia kwa nyumba yao na walipokaribia na kuingia ndani wakampata mkewe pia amefariki.

Muhtasari

• “Kunafikiriwa kwamba amepigwa na nyundo kwa sababu kulikuwepo na nyundo pale kando ya mwili wake."

Mume amgonga mkewe kichwani kwa nyundo nzito kabla ya kujitia kitanzi.
Gari la polisi Mume amgonga mkewe kichwani kwa nyundo nzito kabla ya kujitia kitanzi.
Image: Screengrab//

Mwanamume wa miaka 58 ameripotiwa kumuua mke wake kwa kumpiga nyundo nzito kichwani kabla yake pia kujitoa uhai kwa kujitia kitanzi katika eneo la Mathira kaunti ya Nyeri.

Kwa mujibu wa ripoti kwenye runinga ya Citizen, wapiti njia waliona mwili wa Dedan Gachoka ukiwa umening’inia nje ya nyumba yao kabla ya kumpata mkewe Judy Wangui naye akiwa ameuawa ndani ya nyumba hiyo.

Kamanda wa polisi eneo hilo Benjamin Rotich alisema kuwa mama huyo aliyekuwa katibu wa nyumba kumi na mhudumu wa afya wa kujitolea aliuawa kwa kugongwa na kifaa butu kichwani japo chanzo cha mauaji hayo kimesalia kuwa kitendawili kikuu ambacho kitahitaji muda Zaidi kuteuliwa.

“Kunafikiriwa kwamba amepigwa na nyundo kwa sababu kulikuwepo na nyundo pale kando ya mwili wake. Tulipata damu nyingi imemwagika pale na alikuwa amefunikwa na wakati hilo blanketi lilitolewa tulipata kwamba alikuwa amegongwa na kifaa kizito tena butu kichwani,” mmoja wa wanakijiji waliojawa na mshangao walisema.

Wanakijiji walisema kuwa marehemu mke huyo amekuwa katika mstari wa mbele kushiriki katika huduma ya afya katika mitaa kwenye kaunti huyo lakini pia na kutoa ushauri nasaha kuhsu afya ya akili.

Wengine walisema kuwa katika siku za hivi karibuni mume wake amekuwa akionekana nyumbani, wakikisia kwamba huenda alipoteza kazi ila hilo haliwezi kuwa sababu ya mara moja kukisia kuwa ndicho chanzo cha mauaji hayo.