Mahakama yakataa ombi la serikali kupinga uamuzi wa kusitisha kutekelezwa sheria ya fedha

Jaji Thande anasema serikali haikutoa sababu za kutosha kumtaka aondoe amri hizo.

Muhtasari

• Jaji Mugure Thande ametupilia mbali ombi la serikali iliyotaka kutupilia mbali agizo alilokuwa ametoa la kusitisha kutekelezwa sheria ya fedha.

• Katika ombi lake, Waziri wa Hazina Njuguna Ndung’u ameitaka mahakama kutupilia mbali maagizo hayo.

Mahakama
Mahakama
Image: MAHAKAMA

Jaji Mugure Thande ametupilia mbali ombi la serikali la kutupilia mbali agizo alilokuwa ametoa la kusitisha kutekelezwa kwa sheria ya fedha.

Jaji Thande anasema serikali haikutoa sababu za kutosha kumtaka aondoe amri hizo.

Agizo hilo limeongeza muda wa kusubiri kusikilizwa na kuamuliwa kwa kesi hiyo.

Jaji huyo pia ametuma faili hiyo kwa Jaji mkuu ili kumpa jopo kusikiliza ombi hilo kusikiliza kesi hiyo ilyowasilishwa na seneta wa Busia, Okiya Omtata.

Mahakama Kuu jijini Nairobi wiki jana ilikuwa imeongeza muda wa maagizo yaliyotolewa katika kesi iliyowasilishwa na Seneta wa Busia Okiya Omtatah na Wakili Otiende Omollo ikisubiri kusikilizwa na kuamuliwa.

Katika malalamishi yao, wawili hao wanahoji kuwa serikali haitapata madhara yoyote ikiwa maagizo yataongezwa na maagizo ya kihafidhina kutolewa.

Kwa upande wao wamedai baadhi ya vipengele vinatishia haki ya kumiliki mali, kupata haki kwa Wakenya na kukiuka Katiba ya 2010 kwa ujumla.

Omtatah anasema ombi hilo linaibua masuala makubwa ya sheria na faili hiyo inafaa kutumwa kwa Jaji Mkuu kuteua benchi ya majaji kusikiza na kuamua suala hilo.

Hata hivyo, katika ombi lake, Waziri wa Hazina Njuguna Ndung’u ameitaka mahakama kutupilia mbali maagizo hayo.

Waziri huyo alisema kuwa hii italeta mgogoro wa bajeti kwa serikali.

Gavana huyo wa zamni wa benki kuu ya Kenya alimweleza Jaji Mugure Thande kwamba serikali imeendelea kupoteza Sh578 milioni kila siku za ushuru tangu maagizo hayo kutolewa mnamo Juni 30.