Mkurugenzi wa fedha wa Nairobi hospital adungwa kisu mara 16 hadi kufa

Mkuu wa polisi wa Kilimani, Moss Ndiwa alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo, akisema wapelelezi wanamsaka mshukiwa.

Muhtasari
  • Waliwaomba wanausalama wasiruhusu mtu yeyote kutoka katika nyumba hiyo kuondoka.

Polisi wanachunguza mauaji ya kaimu mkurugenzi wa fedha wa The Nairobi Hospital Erick Maigo ambaye alipatikana amefariki ndani ya nyumba yake akiwa na majeraha 16 ya visu.

Maigo, 40, alipatikana Ijumaa asubuhi akiwa ameuawa katika nyumba yake eneo la Woodley, Nairobi.

Mshambulizi wake, mwanamke ambaye pengine alikuwa amekesha usiku kucha kwenye nyumba hiyo au kuifikia asubuhi alitoroka dakika chache kabla ya polisi kufika.

Mkuu wa polisi wa Kilimani, Moss Ndiwa alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo, akisema wapelelezi wanamsaka mshukiwa.

Majirani katika ghorofa ya Woodley Annex walisema walimsikia Maigo akiugua kwa maumivu.

Waliamua kuuendea mlango wake na kuugonga ndipo akakutana na mwanamke mmoja ambaye aliwajulisha kuwa kila kitu kilikuwa sawa na alikuwa anatafuta funguo ili afungue.

Majirani walimsikia Maigo akiwa bado anaugulia maumivu na kutafuta msaada

Bibi aliyekuwa ndani ya nyumba hiyo alikataa kufungua na kuwafanya majirani kuwatahadharisha usalama katika boma hilo.

Waliwaomba wanausalama wasiruhusu mtu yeyote kutoka katika nyumba hiyo kuondoka.

Kulingana na polisi, walikimbia hadi kituo cha polisi cha Kibra ambapo walitoa ripoti ya shughuli za kutiliwa shaka katika nyumba hiyo

Wakati polisi walipofika eneo la tukio, walimkuta mwanamke huyo anayeshukiwa kuwa peke yake hayupo.

Mlango ulikuwa wazi na mwili wa Maigo ulikuwa umelazwa kwenye dimbwi la damu.

Polisi walisema mwili huo ulikuwa na majeraha 16 ya kuchomwa visu.

Majeraha kumi kati ya hayo yalikuwa kifuani na upande wa nyuma. Haijulikani ikiwa mwanamke huyo alitenda peke yake.

Mwili wa Maigo ukahamishwa hadi chumba cha kuhifadhia maiti.

Mauaji hayo yanajiri kabla ya mkutano mkuu wa mwaka uliopangwa wa hospitali hiyo.

Polisi walisema wanachunguza mauaji na wanamsaka mshukiwa ambaye bado hajajulikana.

Sababu ya mauaji hayo bado haijajulikana.