MCK yalaani vikali mashambulizi dhidi ya wanahabari watatu

Mkurugenzi Mkuu Mtendaji David Omwoyo alisema watatu hao walishambuliwa walipokuwa wakiangazia oparesheni ya usalama

Muhtasari
  • Omwoyo alisema uhuru wa vyombo vya habari ni nguzo ya msingi ya demokrasia na ni muhimu kwa wanahabari kutekeleza kazi zao bila kuogopa vurugu au vitisho.
Mkurugenzi mkuu wa MCK, David Omwoyo
Image: MCK (Facebook)

Baraza la Vyombo vya Habari nchini Kenya limelaani shambulizi dhidi ya wanahabari wa televisheni katika kaunti ya Machakos siku ya Jumatatu na kuwataka polisi kuharakisha uchunguzi na kuwafungulia mashtaka watu waliohusika.

Katika taarifa yake Jumanne, Mkurugenzi Mkuu Mtendaji David Omwoyo alisema watatu hao walishambuliwa walipokuwa wakiangazia oparesheni ya usalama katika shimo la kutengenezea pombe haramu huko Matungulu.

“Wanahabari Mike Ndunda kutoka Kamba TV, Richard Muasya wa Athiani FM na Boniface Mutisya wa Mutongoi TV walikuwa wamealikwa kuangazia uvamizi uliofanywa katika eneo la Katine na Chifu wa eneo hilo Francis Mulinge na kushambuliwa na kundi la watu walipokuwa wakirekodi operesheni hiyo. "

Omwoyo alisema uhuru wa vyombo vya habari ni nguzo ya msingi ya demokrasia na ni muhimu kwa wanahabari kutekeleza kazi zao bila kuogopa vurugu au vitisho.

Alisema vyama vinavyohisi kukerwa na vyombo vya habari vitoe taarifa kwa Tume ya Malalamiko, chombo kilichopewa mamlaka kisheria kusuluhisha suala hilo badala ya kujichukulia sheria mkononi.

"Mashambulizi dhidi ya waandishi wa habari sio tu kwamba yanakiuka haki zao za kimsingi za binadamu bali pia yanadhoofisha kanuni za uhuru wa kujieleza na majadiliano ya wazi ambayo ni muhimu kwa jamii yenye afya njema. Tunaziomba mamlaka zetu za kusimamia sheria kuchukua hatua za haraka na madhubuti za kuchunguza na kuwashtaki waliohusika na haya. mashambulizi,” Omwoyo alisema.

Haki za wanahabari zinalindwa na sheria chini ya Katiba na Sheria ya Baraza la Habari ya mwaka 2013.