logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Imani ya waumini yadaiwa kusababisha vifo vya watoto wawili

Waumini wa Kanisa la Mungu Neno la Kweli  kilifi hawaamini kwenda hospitalini

image
na

Habari22 September 2023 - 06:19

Muhtasari


•Polisi Kilifi Kaskazini  wanawazuilia washukiwa 11 ili kukamilisha uchunguzi wa vifo vya watoto wawili.

Itikadi kali? Baadhi ya waumini wa Kanisa la Mungu neno la Kweli walipofikishwa katika mahakama ya Kilifi kwa ajili ya kutoa uamuzi wa maombi ya polisi ya kuwataka washikiliwe kwa siku 14. Picha: ELIAS YAA

Mahakama ya Kilifi imewapa polisi hadi Jumatatu kuwashikilia washukiwa 11 kuhusiana na vifo vya watoto wawili wanaodaiwa kufariki kutokana na mafundisho ya kidini.

Hakimu mkuu wa Kilifi Justus Kituku siku ya Alhamisi aliamua kwamba 11 hao ambao ni pamoja na wazazi wa marehemu wanapaswa kuendelea kuzuiliwa na polisi hadi Jumatatu ambapo polisi wanatarajiwa kutoa ripoti yao.

Kituku alisema ingawa ni haki kwa mujibu wa Ibara ya 49 ya katiba kwa mshtakiwa kupewa bondi, baadhi ya mazingira yanaweza kusababisha mahakama kuwanyima dhamana.

“Mambo kama vile utata wa suala linalochunguzwa, upeo wa upelelezi, uzito wa kosa linalochunguzwa, uhusiano wa watu waliokamatwa na wahasiriwa, na wanaotarajiwa kuwa mashahidi. Katika kisa hiki, kuna madai ya mafundisho ya itikadi kali yaliyosababisha vifo vya watoto, na kama tumejifunza kutoka kwa suala la Shakahola, uchunguzi huu unaweza kuwa mpana," ilisoma sehemu ya uamuzi huo.

Polisi wanaamini kuwa watoto hao wenye umri wa miaka 11 na 13 walifariki baada ya wazazi wao kukosa kuwapeleka hospitalini kutokana na imani ya kanisa lao.

Ni washiriki wa Kanisa la Mungu Neno la Kweli linaloamini katika uponyaji wa kimungu. Waumini wa kanisa hilo hawaamini kwenda hospitalini bali huomba tu wakati mtu anakuwa mgojwa.

Kamanda wa polisi wa Kaunti Ndogo ya Kilifi Kaskazini Kenneth Maina alisema mmoja wa watoto hao alifariki Jumamosi nyumbani kwao. Wa pili alifariki siku ya Jumapili nyumbani kwa muumini wa kanisa hilo.

"Tulipata habari kutoka kwa umma siku ya Jumapili kuhusu kifo kinachoshukiwa cha mtoto mdogo na watu walikuwa wakipanga kuficha kifo hicho'.polisi walisema

Tulifanikiwa kufika mahali walipokuwa wamekusanyika lakini watoto walikuwa wamefukuzwa. Mwili wa mtoto pia ulikuwa umetolewa.

Tuliwakamata wengine na kwenda kwenye boma la wazazi ambapo tuliwakamata wengine. Kufikia wakati huo wazazi walikuwa hawajajua kifo cha mtoto wa pili,” alisema. Maina alisema dini hiyo haina jengo la kimwili ambapo wanafanyia ibada zao bali kila Jumapili hukusanyika katika kiwanja cha mwanachama yeyote atakayejitolea kuwakaribisha.

“Ni changamoto kuwafuatilia kwa sababu hawana kanisa. Kila wakati huduma yao inafanywa katika eneo tofauti ambalo linaweza kuwa hata mji tofauti.

  Polisi waliomba kuwazuilia washukiwa hao ili uchunguzi wa maiti ufanyike.

 


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved