Polisi wa AP Lilian Biwott aliyempiga risasi na kumuua mumewe Eldoret kuzuiliwa kwa siku 14

Wanandoa hao wana watoto watatu na msaidizi wa nyumba ambao walikuwepo wakati wa tukio hilo.

Muhtasari
  • Nzau alisema katika hati ya kiapo kwamba pia wanahitaji muda wa kurekodi taarifa kutoka kwa mashahidi muhimu.

Polisi wamepewa siku 14 kumshikilia polisi wa utawala Lilian Biwott aliyempiga risasi mumewe mjini Eldoret.

Afisa wa DCI Stephen Nzau alimweleza Hakimu Mkuu Dennis Mikoyani kwamba walihitaji muda kufanya uchunguzi wa mwili wa marehemu Victor Kipchumba.

Nzau alisema katika hati ya kiapo kwamba pia wanahitaji muda wa kurekodi taarifa kutoka kwa mashahidi muhimu.

"Silaha ya mauaji ni bunduki aina ya AK 47 ambayo bado haijachukuliwa kwa uchunguzi wa balestiki pamoja na risasi zilizotumika," alisema Nzau.

Alipoulizwa iwapo anakubaliana na maombi ya kumshikilia kwa siku 14, Lilian alisema hana tatizo na hilo.

Mikoyani aliagiza azuiliwe katika kituo cha polisi cha Eldoret Central na awasilishwe kortini katika muda huo.

Lilian alionekana ametulia kizimbani siku mbili baada ya kujiwasilisha kwa polisi kufichua kuwa alimuua kwa kumpiga risasi mumewe.

Kisa hicho kilitokea Kimumu Estate ambapo wanandoa hao waliishi katika nyumba ya kupanga.

Wanafamilia walisema kwamba wawili hao walikuwa wametishia kuuana kwa madai ya kuwa na mzozo wa kimapenzi ambao ulitikisa uhusiano wao.

Wanandoa hao wana watoto watatu na msaidizi wa nyumba ambao walikuwepo wakati wa tukio hilo.