Migori: Rushwa ya ngono kwa ajili ya kupata samaki imechangia maambukizi ya UKIMWI

Baadhi ya wanawake wanaofurika katika fukwe za ziwa Victoria hawapendi kujihusisha kimapenzi na wavuvi kwa kupenda kwao bali ni kwa kukosa cha kulipa Nzaidi ya rushwa ya ngono tu ili kupata samaki

Muhtasari

• Obiero alisema wamewashauri wavuvi kutumia njia zilizopo za kuzuia kwa sababu wengi wao bado wako katika hatari kubwa ya kupata UKIMWI.

Maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI katika fukwe za ziwa Victoria haswa kaunti ya Migori yamechangiwa na kukithiri kwa visa vya rushwa ya ngono kwa ajili ya kupata samaki.

Haya ni kwa mujibu wa Kituo cha Kimataifa cha Afya, Elimu, na Usalama wa Mazingira (CIHEB).

Ripoti iliyochapishwa na Citizen ilisema kwamba mratibu wa program hiyo kwa ajili ya wavuvi katika fukwe za kaunti ya Migori Peter Obiero alisema kwamba visa vya kubadilishana ngono kwa ajili ya kupata samaki bado vinashuhudiwa katika kaunti hiyo.

Baadhi ya wanawake wanaofurika katika fukwe za ziwa Victoria huwa hawapendi kujihusisha kimapenzi na wavuvi kwa kupenda kwao bali ni kwa kukosa cha kulipa Nzaidi ya rushwa ya ngono tu ili kupata samaki, Obiero alisema.

Alisema wameweza kufanya uhamasishaji katika fukwe na sasa idadi ya wanawake wanaojihusisha na mapenzi kwa ajili ya samaki sasa inashuka kwa hisani ya uwezeshaji huo.

Obiero alisema wamewashauri wavuvi kutumia njia zilizopo za kuzuia kwa sababu wengi wao bado wako katika hatari kubwa ya kupata UKIMWI.

Naibu mratibu wa udhibiti wa UKIMWI Kaunti ya Migori Caroline Odera alisema idara ya afya inashirikiana kwa karibu na washirika ili kupunguza visa vya maambukizi ya VVU miongoni mwa jamii ya wavuvi.

Odera alisema jamii ya wavuvi bado iko katika hatari kubwa ya kupata VVU katika kaunti hiyo. Ametoa wito kwa wale walio katika hatari kutumia njia za kuzuia VVU.