KMPDU yashikilia msimamo wao licha ya serikali kukubali kutekeleza matakwa yao 18 kati ya 19

Kwa mujibu wa Atellah, ni heri serikali ikatae kutekeleza matakwa hayo 18 na kulitekeleza hilo moja tu ambalo waliacha nje – suala la madaktari wanagenzi.

Muhtasari

• Madaktari wamekuwa kwenye mgomo kwa Zaidi ya mwezi wakieleza malalamiko yao kwa serikali kuu na serikali za kaunti kutaka kutekelezwa kwa mkataba wa maelewano ya mwaka 2017.

Dr Davji Bhimji Attelah
Dr Davji Bhimji Attelah
Image: FACEBOOK//Dr Davji Bhimji Attelah

Katibu mkuu wa muungano wa wahudumu wa afya, KMPDU Devji Atellah amejibu baada ya serikali kusema kwamba imekubali kutekeleza matakwa 18 kati ya 19 ambayo wahudumu wa afya wamekuwa wakidai kwa wiki 5 sasa.

Madaktari wamekuwa kwenye mgomo kwa Zaidi ya mwezi wakieleza malalamiko yao kwa serikali kuu na serikali za kaunti kutaka kutekelezwa kwa mkataba wa maelewano ya mwaka 2017.

Madaktari hao wamekuwa wakipinga vikali hatua ya serikali kupunguza mshahara wa madaktari wanagenzi kutoka kima cha shilingi 206k hadi 70k kwa mwezi, jambo ambalo serikali imekuwa ikisema kuwa hatua hiyo ni kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya madaktari wote.

Hata hivyo baada ya serikali kukubali kutekeleza matakwa 18 kati ya 19, katibu Atellah amekataa kutoa tangazo kwa madaktari kurejea kazini.

Kwa mujibu wa Atellah, ni heri serikali ikatae kutekeleza matakwa hayo 18 na kulitekeleza hilo moja tu ambalo waliacha nje – suala la madaktari wanagenzi.

“Ndugu Serikali, madaktari wanasema kwa vile mmesema hadharani kwamba mlikubali matakwa yetu 18 kati ya 19 (isipokuwa suala la wanagenzi), tafadhali rudisha 18 na mtupe 1. Kama jamii, hatujazoea kuacha Zaidi walio katika mazingira magumu, na kwetu sisi, wanagenzi kwa sasa wako hatarini sana,” Atellah alisema kupitia ukurasa wake wa X.

Tangu mgomo huo ulipoanza mwzi jana, mazungumzo baina ya KMPDU na serikali yamekuwa yakigonga mwamba mara kwa mara, huku mkuu wa utumishi wa umma, Felix Koskei akiwataka kurejea kazini na waziri wa afya Susan Nakhumincha akisisitiza kwamba serikali haiwezi kutekeleza matakwa yao yote kwa wakati mmoja.

Baadhi ya serikali za kaunti zimetoa tangazo la kuwasimamisha kazi madaktari wanaogoma.