Kigame awakosoa rais Ruto na naibu wake Rigathi Gachagua

Aliwashutumu wanasiasa hao kwa kuwagawanya Wakenya kwa misingi ya kikabila.

Muhtasari

•"Wanajaribu kutufanya tuzungumze kuhusu mgawanyiko wao, wakati masuala ya kweli ni mateso ya Wakenya kufukuzwa, kubomolewa na pia mswada wa Fedha."

•Kuhusu Muswada wa Sheria ya Fedha, Kigame alitoa changamoto kwa Wabunge kuhakikisha ushirikishwaji wa wananchi ipasavyo.

Ruben Kigame
Ruben Kigame
Image: Facebook//Ruben Kigame

Aliyekuwa mgombea urais Reuben Kigame amemkashifu Rais Wiliam Ruto na naibu wake Rigathi Gachagua kwa kile alichodai wanahubiri umoja wa kitaifa, lakini matendo yao yanaonekana kuwa tofauti.

Akizungumza katika kipindi cha Daybreak cha Citizen TV Kigame alikashifu tabia za viongozi hao wawili, akisema vitendo vyao vimesababisha mgawanyiko nchini.

“Mzigo wa ushahidi wa umoja wa kitaifa uko kwa wawili hao, wawili hao waungane kisha watuambie tuungane. Huwezi kuwa unacheza siasa za kikabila kama Rigathi na kuteua watu kulingana na kabila kama Ruto. Halafu unatuhubiria kuhusu umoja wa kitaifa, huo ni unafiki,” Kigame alisema

Kulingana na Kigame, mazungumzo ya hivi majuzi kuhusu mgawanyiko kati ya Ruto na Gachagua yanalenga kuelekeza hisia za taifa kutoka kwa masuala halisi yanayowasumbua Wakenya.

"Wanajaribu kutufanya tuzungumze kuhusu mgawanyiko wao, wakati masuala ya kweli ni mateso ya Wakenya kufukuzwa, kubomolewa na pia mswada wa Fedha."

Alishutumu wanasiasa hao kwa kuwagawanya Wakenya kwa misingi ya kikabila.

Mwanamuziki huyo pia amemkashifu Ruto kwa kile alichokitaja kuwa ukosefu wa uwazi katika gharama ya kukodisha ndege ya kibinafsi wakati wa ziara yake nchini Marekani.

“Rais anaposema tunatakiwa kuishi kulingana na uwezo wetu lakini yeye mwenyewe anatumia muda wake kusafiri kupita kiasi, akitumia pesa za aina hiyo na kudanganya jumuiya ya kimataifa. Kulala kwenye mkutano wa maombi. Kuna utata kwenye gharama za safari,” alisema.

Kuhusu Muswada wa Sheria ya Fedha, Kigame alitoa changamoto kwa Wabunge kuhakikisha ushirikishwaji wa wananchi ipasavyo.

Alikashifu bunge kwa kushindwa kuhakikisha kuwa Mswada huo unafikiwa na wananchi wote, kwa mapitio na kuwasilishwa kwa memoranda.

Kwa mfano, watu wanaoishi na ulemavu wametengwa, kwa vile mswada haujaweza kupatikana katika miundo kama vile braille na lugha ya ishara.

Kigame alitoa changamoto kwa wabunge kuchukua hatua binafsi ya kuwasilisha mswada huo kwa wapiga kura wao na kupata maoni yao.