Watu watano wafariki kwenye ajali kwenye barabara ya Gilgil-Naivasha

Takriban wengine 19 walijeruhiwa katika ajali hiyo iliyotokea eneo la Kigio iliyohusisha matatu tatu mwendo wa saa nane usiku

Muhtasari

•Waliofariki ni wanaume wawili, mwanamke, mvulana na msichana huku idadi ikihofiwa kuongezeka.

•Miili hiyo ilipelekwa katika hifadhi ya maiti ya hospitali ya kaunti ndogo ya Gilgil huku waliojeruhiwa wakiendelea kupata matibabu katika hospitali ndogo ya kaunti ya Naivasha.

Ajali
Ajali
Image: HISANI

Takriban watu watano walifariki Alhamisi 27 usiku katika ajali iliyotokea kwenye barabara ya Gilgil-Naivasha.

Kulingana na  polisi takriban wengine 19 walijeruhiwa katika ajali hiyo iliyotokea eneo la Kigio iliyohusisha matatu tatu mwendo wa saa nane usiku. Waliojeruhiwa walikimbizwa hospitalini wakiwa na majeraha mengi.

Waliofariki ni wanaume wawili, mwanamke, mvulana na msichana. Kuna hofu kwamba huenda idadi ya vifo ikaongezeka, polisi walisema wakitaja athari za ajali hiyo.

Kulingana na polisi na mashahidi, kisa hicho kilihusisha matatu ya kampuni ya Narok Line Services, matatu ya Mau Narok Sacco na nyingine ya Ennus Matatu Sacco.

Polisi walisema gari moja lililohusika katika ajali hiyo lilikuwa likivuta lingine kutoka Naivasha kuelekea Gilgil kabla halijatokea. Matatu iliyokuwa ikija ilichukua kundi la magari na kushindwa kurejea kwenye njia yake kwa wakati, mashahidi na walionusurika waliambia polisi.

Dereva alishindwa kulidhibiti gari hilo na kuligonga jingine ubavuni alipojaribu kuungana na njia yake kabla ya kubingirika mara kadhaa na kusababisha vifo hivyo.

Waliojeruhiwa wanaendelea na matibabu katika hospitali ndogo ya kaunti ya Naivasha. Miili hiyo ilipelekwa katika hifadhi ya maiti ya hospitali ya kaunti ndogo ya Gilgil.

Hii ndio ajali mbaya ya hivi punde katika barabara kuu ambayo imegharimu maisha ya watu wengi na kuwaacha mamia ya wengine na majeraha mabaya.