NPS yazungumzia madai ya polisi wa Kenya kuuawa Haiti

Kundi la kwanza la maafisa wa polisi wa Kenya wapatao 400 waliwasili Haiti mnamo Juni 25.

Muhtasari

•Huduma ya kitaifa ya polisi imepuuzilia mbali ripoti kuhusu maafisa wa polisi waliotumwa nchini Haiti kuuawa.

•Picha ya ripoti zisizothibitishwa ilisambazwa hivi majuzi kwenye mitandao ikidaiwa kuwa maafisa saba wa polisi wameuawa.

Image: Kithure Kindiki / X

Idara ya kitaifa ya Huduma kwa polisi ,NPS imepuuzilia mbali ripoti kwamba baadhi ya maafisa wake waliotumwa Haiti kwenye misheni ya kulinda amani inayoungwa mkono na umoja wa mataifa wameuawa.

Hii ilikuwa baada ya madai kuibuka mtandaoni kwamba maafisa saba waliuawa katika taifa hilo lililokumbwa na vita la visiwa vya Caribbean huku magenge yenye silaha yakizidisha shinikizo dhidi ya wanapolisi waliotumwa.

Picha iliyosambazwa sana mwishoni mwa wiki iliyopita ilionyesha picha ya hivi majuzi ya polisi wa Kenya waliokuwa wakishika doria katika mji mkuu wa Haiti Port-au-Prince, ikiwa na maandishi yanayodai kuwa maafisa hao wa Kenya wameripotiwa kufariki.

"Polisi 7 wa Kenya waliripotiwa kufariki Haiti aki [Rais William Ruto] Mungu hatakusamehe kamwe," maandishi yalisomeka.

Hata hivyo,huduma ya kitaifa ya polisi ilitaja picha hiyo kuwa ya uwongo na mbali na hayo haikutoa taarifa zaidi kuhusu misheni hiyo au hali ya wanapolisi wa Kenya.

Kundi la kwanza la maafisa wa polisi wa Kenya wapatao 400 waliwasili Haiti mnamo Juni 25 huku kundi lingine likisubiriwa kutua nchini humo.

Rais wa Kenya William Ruto alikuwa amewahutubia polisi wakiondoka siku moja mapema jijini Nairobi, katika kile alichoeleza kama dhamira ya "kihistoria" ya mshikamano.