Aliyekuwa gavana wa Nairobi Mike Sonko sasa amemtaka naibu rais Gachagua kumheshimu bosi wake na akome kumhujumu kwa manufaa ya chama cha Kenya Kwanza.
Akizungunmza katika mahojiano aliwashauri viongozi wa mrengo wa Kenya Kwanza kutopigana hadharani kwani sio mfano kwa wapiga kura wao.
“Kile serikali inachofanya sasa hivi ni makosa hata mbele ya wadogo wao. Hupigani hadharani, umepigiwa kura mnapigania nini mbele ya watu, unajaribu kuwaonyesha Wakenya nini. Watu waheshimiane,” Sonko alidai.
Gavana huyo wa zamani aliendelea kusema kuwa Rais anafaa kuheshimiwa na naibu wake ili wabunge wadumishe umoja.
“Rais aheshimiwe kama rais, naibu wa kuinua heshima yake kutoka kwa wabunge. Kama naibu wa kuongeza makosa, anyenyekee amwambie rais pole, nilidhani wewe ndio ulituma hawa watu wanitupie maneno,” Mike Sonko alisema.
Akizungumzia masuala ya ndani kama chama, Sonko alisema hakutakuwa na heshima ndani ikiwa kiongozi wa chama ambaye ni Rais Ruto hataheshimiwa.
“Wao kama Kenya Kwanza waheshimiane. Heshima kwa Kenya Kwanza haiwezi kuwa kama kiongozi wa chama wao hawajapewa heshima. Mambo ya ndani kama Kenya Kwanza lazima wamheshimu rais.”
"Gachagua lazima amheshimu rais, asimhujumu bosi wake, akiwa amedhoofisha, wabunge wataanza kupeana maneno, lakini bosi ni nani?" aliweka.
Mfanyibiashara huyo aliongeza kuwa Naibu Rais Gachagua lazima asimhujumu bosi wake. Alisema wote wana wabunge wanaounga mkono na iwapo Gachagua atamdharau Ruto, wataanza kunyoosheana vidole.
Mike Sonko awali alikuwa ameshutumu watu walio karibu na rais kwa ujinga wao na ubinafsi wao, akiongeza kuwa alionya kuhusu hili hapo awali.
Aliteta kuwa Rais Ruto sio tatizo na sababu ya machafuko yanayoshuhudiwa nchini hivi leo, lakini watu wake wa karibu ndio.