Shollei atilia shaka dawa hatari za kuua wadudu shambani zinazouzwa kwa wakulima nchini

Naibu spika huyo anahisi matumizi ya dawa hizi hatari shambani yamechangia kwa ongezeko la visa vya gonjwa la saratani ya aina mbalimbali nchini.

Muhtasari

•Alikosoa Bodi ya Kudhibiti dawa za kuua wadudu shambani kwa kushindwa kuboresha orodha ya dawa hizo zinazoruhusiwa, hali ambayo imeruhusu vitu hivi hatari kuendelea kupatikana kwa urahisi.

•Alikumbuka kupokea vitisho kutoka kwa nguvu kubwa za kampuni za dawa za kuua wadudu shambani wakati wa kampeni yake dhidi ya dawa hizi.

NAIBU SPIKA GLADYS SHOLLEI
Image: EZEKIEL AMING'A

Naibu Spika wa Bunge la Kitaifa, Gladys Boss Shollei, amezua tahadhari na taharuki kuhusu usambazaji wa dawa hatari za kuua wadudu shambani nchini Kenya, akihusisha matumizi yao na kuongezeka kwa visa vya saratani.

Shollei amekosoa uagizaji wa dawa za kuua wadudu shambani zilizopigwa marufuku katika nchi za Magharibi, akijiuliza kwa nini mamlaka za Kenya hazijachukua hatua kuondoa bidhaa hizi hatari sokoni licha ya hatari zao zinazojulikana kwa siha na maumbile ya wanadamu.

Katika kikao cha bunge kilichofanyika Jumanne, Shollei alisisitiza matokeo ya ripoti ya "The Pesticide Atlas," iliyoandaliwa na wanasayansi 20 kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi, ambayo ilifunua kuwa dawa 267 zilizopigwa marufuku barani Ulaya na Marekani bado zinatumika nchini Kenya.

Alikosoa Bodi ya Kudhibiti dawa za shambani kwa kushindwa kuboresha orodha ya dawa zinazoruhusiwa, hali ambayo imeruhusu vitu hivi hatari kuendelea kupatikana kwa urahisi.

Shollei, ambaye anawakilisha Kaunti ya Uasin Gishu, alidai kuwa Bodi ya Kudhibiti dawa za kuua wadudu shambani na Wizara ya Kilimo zimeathiriwa na kampuni za dawa hizo, ambazo anaamini zimesababisha kuachwa kwa bidhaa hizi hatari kusambaa.

Alisema kuwa watengenezaji kutoka Marekani na Ulaya wanaendelea kuuza kemikali hizi hatari nchini Kenya licha ya madhara yao kuwa bayana na wazi.

Alitaja kesi maarufu nchini Marekani ambapo mkulima alilipwa dola milioni 250 baada ya kupata saratani kutokana na matumizi ya dawa moja ambayo pia inauzwa Kenya kwa majina tofauti.

Alisema kuwa kesi hiyo inadhihirisha hatari kubwa zinazohusiana na dawa hizi.

Shollei aliwasihi wabunge kuchukua hatua kwa haraka iwezekanavyo, akionya kwamba wabunge watakuwa na hatia ikiwa watashindwa kuchukua hatua mwafaka kwa suala la dharura kama hili.

Alikumbuka kupokea vitisho kutoka kwa nguvu kubwa za kampuni za dawa za kuua wadudu shambani wakati wa kampeni yake dhidi ya dawa hizi, akisisitiza umuhimu wa hatua za kisheria za haraka ili kuzuia madhara zaidi kwa wananchi wa Kenya.

Katika wito wake kwa wanasheria wenzake, Shollei alisisitiza umuhimu wa kushughulikia chanzo cha saratani badala ya kuwekeza tu katika matibabu, na kuonyesha dharura ya hali hiyo.