"Lazima mtakiona cha mtema kuni" - Duale awambia Makamishna waasi wa IEBC

“Hapana haiwezi kuwa biashara kama kawaida!" - Aden Duale

Muhtasari

• "Kwa hiyo, makamishna hao wanne wanapaswa kuwajibika kibinafsi na kwa pamoja,” Duale alisema.

Mbunge Aden Duale amesema makamishna waasi wa IEBC lazima wakione cha mtema kuni
Mbunge Aden Duale amesema makamishna waasi wa IEBC lazima wakione cha mtema kuni
Image: Facebook, Maktaba

Mbunge wa Garissa Mjini Aden Duale amesisitiza msimamo wake kwamba makamishna wanne waliojitenga na matokeo ya tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC ni sharti watakiona cha mtema kuni kwa njia yoyote ile.

Akiachia maoni yake zaidi ya kumi kwenye ukurasa wake wa Twitter kuhusu ni kwa nini makamishna hao lazima waadhibiwe, Duale alisema hata wajikengeushe aje, Wakenya si wajinga wa kupelekwa kama upepo wa kimbunga.

Duale alikemea hatua ya makamishna hao waasi kukengeuka ghafla na kusema wanaunga mkono ripoti ya mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati kwamba matokeo yalikuwa ya halali, siku moja tu baada ya mahakama kuhakikisha hilo, jambo ambalo awali walijitenga nalo kwa kusema kwamba uchaguzi ulikumbwa na msukosuko.

Alisema kitendo hicho kinawaonesha kama lumbwi anayebadilika rangi kulingana na mazingira hakifai kwani hao wanne ndio walichangia nusra taifa litumbukie kwenye mzozo wa vita vya wenyewe kwa wenyewe mnamo Agosti 15 wakati wa kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi wa urais.

“Hawa ni Makamishna walewale waliotazama moja kwa moja kwenye kamera bila kupepesa macho na kutoa taarifa za uongo kuwa uchaguzi haukuwa na mvuto na mtu mmoja anaonyesha tu kudharau mchakato wa uchaguzi na kupindua ushindi wa wazi wa Rais wetu Mteule MHE. @WilliamsRuto. Hawa ni Makamishna haohao waliotoka Bomas baada ya kushawishiwa na "vigogo" wao kudharau matakwa ya wananchi!” Duale alifoka.

Aliuliza kwamba sasa ni nini kimefanyika ambapo ghafla wanajihusisha na uwazi wa matokeo hayo ambayo awali waliyakana kuwa yalikuwa yamegubikwa na kiza.

Kwa kuzingtia maswali hayo, Duale alisema kwamba hakuna kitu kitaendelea kwa hali ya kawaida pasi na kuwaadhibu kwa vitendo vyao vya kujaribu kuvuruga matokeo.

“Hapana haiwezi kuwa biashara kama kawaida! Vitendo katika kile kilichoonekana kama sinema inayomshirikisha Cherera kama mwigizaji mkuu na mwigizaji wa sauti ni ukiukwaji wa wazi wa Katiba na sheria kwa kujaribu kupotosha matakwa ya Watu kupitia uzushi. Kwa hiyo, makamishna hao wanne wanapaswa kuwajibika kibinafsi na kwa pamoja,” Duale alisema.