logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mimi sio mtu wa kichini chini, Nikitaka kukutana na Ruto naweka wazi - Kalonzo

"Mimi sio mtu wa kichini chini. Nikitaka kukutana na Ruto nitakutana na yeye wazi baada ya kufanya mazungumzo na chama chetu" - Kalonzo

image
na Radio Jambo

Habari11 September 2022 - 05:18

Muhtasari


• Kiongozi huyo wa Wiper alisema yeye anafurahia kuhudumu kutoka upinzani na wala hajakutana na Ruto.

• Alisema picha zinazosambazwa akiwa nac Ruto ni za 2018 alipopoteza babake.

Kalonzo Musyoka wakilonga na William Ruto

Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka amepuuzilia mbali uvumi kwamba yumo mbioni kujiunga mrengo wa serikali unayoongozwa na rais mteule William Ruto.

Akizungumza Jumamosi, Kalonzo aliapa kwamba yeye atasalia kwenye mrengo wa upinzani ili kupambana vilivyo na serikali ya Dkt. Ruto.

“Siwezi jali hata kama tutakuwa kwa upinzani, tutasukuma. Tutashinikiza ili bwawa la Yatta litengenezwe na miradi mingine. Hata itakuwa vizuri zaidi kwangu nikiwa upinzani ili kung’ang’ana na watu hawa. Huwa tunasema miaka 5 ni kipindi kifupi sana na tumejitolea kuhudumia Wakenya kutoka upinzani kwa njia mwafaka kulingana na uwezo wetu, na tuko tayari” Kalinzo alisema.

Kiongozi huyo ambaye alikuwa makamu wa rais Kibaki alichukua pia fursa hiyo kumpongeza Ruto na kusema kwamba wanamheshimu licha ya kutokubaliana na matokeo ya kesi ya mahakama ya upeo Jumatatu.

Alipinga vikali madai yanayomhusisha na kushikana mikono na rais mteule William Ruto na kusema kwamba kiongozi huyo wa UDA alikwenda kumuona wakati mmoja alipopoteza babake mzazi na kusema hawana urafiki wa karibu na yeye kama ambavyo imekuwa ikisemekana mitandaoni.

“Kuna wengine walikuwa wanaweka kwa mitandao picha tukiwa na Ruto wakisema Kalonzo amekutana na Ruto. Alikuja kuniona wakati nilipoteza babangu 2018 na hizo picha ndio watu wanatumia mitandaoni. Mimi sio mtu wa kichini chini. Nikitaka kukutana na Ruto nitakutana na yeye wazi baada ya kufanya mazungumzo na chama chetu cha Wiper na Azimio la Umoja One Kenya,” aliongeza.

Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na mfumuko wa wanasiasa kutoka vyama vya upinzani kujiunga na mrengo wa Ruto na mwishoni mwa wiki jana uvumi ulisambazwa kwamba Kalonzo baada ya kujiondoa katika kinyang’anyiro cha spika wa seneti, yumo mbioni kujiunga na Ruto, jambo ambalo alilipuuzilia mbali kabisa Jumamosi katika hafla moja ya mazishi huko kwao Ukambani.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved