Mama wa taifa Rachel Ruto alikuwa gumzo la mitandaoni Alhamisi baada ya kutokea na nguo kama za maafisa wa kulinda misitu wakati wa kuongoza hafla ya upandaji miti kaunti ya Kakamega.
Katika msururu wa picha mama wa taifa alizozipakia kwenye Twitter yake, alionekana amevalia viatu vya kiume aina ya Safari boots na kofia pamoja na sare kama ya afisa wa kulinda misitu na kusema kuwa alifurahi kujumuika na wenyeji wa kaunti hiyo ya Magharibi mwa Kenya kwa mara ya kwanza tangu kuingia kwenye ikulu kama mke wa rais wa tano William Ruto.
Mama taifa alisema kuwa hii wiki ikiwa ni ya kusherehekea siku yake ya kuzaliwa, alijawa na faraja kushiriki mapema katika kuongoza shughuli ya kuleta tija kimazingira.
“Waliokuwepo Mhe. Soipan Tuya (CS, Wizara ya Mazingira na Misitu), Mhifadhi Mkuu wa Misitu Julius Kamau miongoni mwa viongozi wengine na wakazi wa Kaunti ya Kakamega. Nimepokea wito katika wiki ya siku yangu ya kuzaliwa ili kujumuika baada ya Mheshimiwa Rais William kujieleza kuhusu suala la upandaji miti na kuweka shabaha ya miti bilioni 5 katika miaka 5 ijayo, na miti bilioni 10 ifikapo 2032. Wakati mzuri wa kupanda mti ulikuwa miaka ishirini iliyopita. Wakati wa pili mzuri ni sasa,” Mama Rachel aliandika.
Katika hotuba yake siku ya mashujaa, rais William Ruto aliwataka Wakenya kuwa mstari wa mbele katika kulinda mazingira na pia kuwahimiza kupanda miti kila mara ili kufikia mwaka 2032 taifa liwe limekidhi hitaji la misitu nchini ili kukwepa kiangazi.
Pia alisema hivi majuzi kwamba kazi mtaani haitoendelea tena na balada yake vijana waliokuwa wakifanya kazi hiyo watakuwa wanalipwa wakipanda miti.