Mzee afukua mwili wa mkewe uliozikwa 2021, auzika kwingine ili kuuza shamba hilo

Mnunuzi alikataa kununua sehemu iliyo na kaburi, jambo lililomfanya mzee wa miaka 76 kufukua mwili ili kuuzika kwingine.

Muhtasari

• Maafisa wa polisi walifika katika boma hilo na kumtia mbaroni pamoja na washirika wake.

Maktaba
Maktaba
Image: Kaburi

Wakaazi wa kijiji cha Mumero katika kaunti ya Meru walisabahiwa na kisa kisicho cha kawaida baada ya mzee mmoja wa miaka 76 kufukua mwili wa marehemu mke wake ili kuuza kipande hicho cha ardhi ambapo mkewe alizikwa.

Kulingana na taarifa zilizochapishwa na Kenya News, mzee huyo alipatwa na tamaa ya pesa inayosukumwa na njaa jambo lililomzalishia wazo la kupiga mnada kipande cha ardhi.

Lakini kaburi la mkewe likawa kizingiti kikubwa kwani hakuna mnunuzi aliyekuwa tayari kumiliki kipande hicho cha ardhi na hivyo mzee alipata wazo kuwa mbadala wake ni kuhamisha kaburi hilo ili apate kuuza shamba.

Ili kufanikisha jambo lake kwa wepesi, mzee huyo aliyetambulika kwa jina Robert Marangu alitafuta msaada wa wanakijiji wenza ili kufukua mwili wa mkewe na kuuzika kwingineko kupisha eneo hilo kupigwa mnada.

Mkewe aliarifiwa kuzikwa mwaka 2021.

Chifu mkuu wa lokesheni ya Kithithina Lucy Mutwiri alithibitisha kisa hicho akisema ni kisa cha ajabu ambacho kimewaacha wakaazi wakizungumza kwa utulivu na kutoamini.

"Ni jambo lisilo la kawaida ambalo limewahi kutokea katika eneo langu na ndiyo maana wakazi wangu waliniarifu juu ya kile kilichotokea. Nilitembelea eneo la tukio na kukuta kaburi limehamishwa kutoka lilipokuwa awali,” alithibitisha chifu huyo kulingana na taarifa ya Kenya News.

"Aliamua kuuza kipande cha ardhi alichomzika mkewe na alifikiri jambo la busara ni kuuhamisha mwili huo," alisema Bi Mutwiri na kuongeza kuwa mwanamume huyo alisaidiwa kuufukua mwili huo na kuuzika tena kwenye kaburi la kina kirefu kwa kushirikiana na mjukuu wake na majirani wengine wawili.

 

Afisa Mkuu wa Upelelezi wa Jinai (DCI) kaunti ndogo ya Buuri Joseph Wambua alisema watu waliohusika walikamatwa na kupelekwa katika kituo cha polisi cha Timau wakisubiri kufikishwa mahakamani leo.

 

Mkazi mmoja, Pius Mwirigi, alizitaka mamlaka hizo kuhakikisha watuhumiwa hao wanafunguliwa mashtaka ili kukomesha matukio hayo yasitokee siku zijazo.