Mbunge wa UDA akosoa hatua ya serikali kutoa msaada wa chakula kwa kina Magoha

Mbunge huyo alisema kuwa familia hiyo ina uwezo mkubwa wa kumudu hilo na badala yake pesa za chakula hicho zielekezwe kwingine.

Muhtasari

• Mbunge Barasa alitoa changamoto kwa serikali kutumia pesa hizo katika masuala mengine kama kuwalipia watoto wa maskini karo.

• Jumamosi naibu rais Rigathi Gachagua alitanagza serikali kutoa chakula kwa wanakijiji wa Magoha na msaada wa usafirishwaji wa mwili wake.

George Magoha
George Magoha
Image: Maktaba

Mbunge wa UDA Didmus Barasa ameikosoa hatua ya serikali kutoa msaada wa chakula kwa watu wa Gem, nyumbani kwa aliyekuwa waziri wa elimu George Magoha kwa wiki mzima wakati maombolezo yanaendelea hadi pale atakapozikwa.

Jumamosi wakati alipotembelea familia ya Magoha katika boma lao Lavington jijini Nairobi, naibu rasi Rigathi Gachagua alitoa tangazo hilo kuwa serikali itasimamia vyakula kwa wanakijiji kando na kutoa msaada wa helikopta ya jeshi la KDF kuusafirisha mwili wake kutoka Nairobi hadi Gem, kaunti ya Siaya.

Tangazo hilo lilipokelewa kwa njia mseto na baadhi ya watu, huku MCA wa Kileleshwa Robert Alai akisema kuwa tamko la Gachagua kutoa msaada wa chakula ni kama kejeli kwa watu wa Gem kuwa wanaungulia makali ya njaa.

Kupitia ukurasa wake wa Twitter, Barasa ambaye ni mbunge wa Kimilili kupitia tikiti ya UDA alikosoa vikali hatua hiyo huku akihoji kuwa ni kwa nini familia hiyo ipewe msaada hali ya kuwa akaunti zao za benki ni nono.

“Kwa nini Serikali isaidie familia ya Prof. George Magoha? , Kuuliza tu kwa niaba ya Wakenya. Hii ni familia ya Tajiri na Profesa mzuri aliyepumzika ana watoto na wanafamilia ambao yeye alisaidia kupata ajira kushoto kulia na katikati katika maisha yake yote alipokuwa akishikilia nyadhifa za ushawishi. Mkewe pia aliweza kupata utajiri wake na nina uhakika akaunti yake haina shida na kifafa cha kifedha kama kile cha Bw Otieno na Wanjiku (mtu wa chini),” Barasa alihoji.

Mbunge huyo mwenye utata alizidi kuelezea kuwa Magoha, kinyume na watu wengine wengi ambao hawajiwezi, alifariki bila kuacha bili kubwa ya matibabu kama ambavyo wengi wa mahasla huacha familia zao zikililia usaidizi huku miili ya wapendwa wao ikishikiliwa katika makafani.

“Kile ambacho familia ya Magoha inahitaji ni chakula na wana uwezo wa kukimudu. Iwapo pesa hizo zinapatikana Serikali inapaswa kuwalipia karo watoto wasiojiweza kutoka Kaunti ya Siaya au Kufuta bili za matibabu kwa Wakenya ambao wako watumwa hospitalini kwa kukosa kulipa bili za matibabu.”