Vijana wetu wameisha kwa sababu ya pombe haramu-DP Gachagua

Gachagua alikuwa akizungumza siku ya Ijumaa mjini Nyeri kwenye mkutano wa kushughulikia suala la unywaji wa pombe haramu.

Muhtasari
  • Alisema aliaibika na maneno ambayo wanawake wanamwambia,huku akisema kwamba vijana wengi wameisha kutokana na pombe haramu.
NAIBU RAIS RIGATHI GAHAGUA
Image: HISANI

Naibu Rais Rigathi Gachagua amesema akina mama wamekashifu tishio la ulevi na pombe haramu.                                                                                   

Alisema aliaibika na maneno ambayo wanawake wanamwambia,huku akisema kwamba vijana wengi wameisha kutokana na pombe haramu.

“Vijana wetu wameisha, badala ya kulala kitandani wanalala chini,” alisema.

Alisema hata shuleni mtu atakuta vyumba vya madarasa vikiwa vitupu kwani hakuna watoto.

"Kwa sababu hii ethanol inakuja huku ikiwa imechanganywa, inamaliza mifumo yote kwa vijana wetu. Betri zote ziko chini ata ikiekwa chaji haiwezi kuchukua. Kwa hiyo wanawake wetu wanalia," alisema.

Ili kukabiliana na tishio hilo, Gachagua alisema serikali itaweka mbinu na mikakati ya kukomesha tishio hilo kuanzia eneo la Kati na kwamba itaweka kasi hiyo kwa nchi nzima.

Gachagua alikuwa akizungumza siku ya Ijumaa mjini Nyeri kwenye mkutano wa kushughulikia suala la unywaji wa pombe haramu.

"Baada ya mkutano huu, haitakuwa kama kawaida, lazima tufanye haki, tutekeleze sheria, na tutimize kiapo cha ofisi. Hatuwezi kuwa sehemu ya kikundi cha uhalifu kinachouza dawa za kulevya. kwa watoto wetu," Gachagua alisema.

Alisema polisi na machifu wanapaswa kufanya kazi yao ya kukomesha tishio hilo na sio kushirikiana na wafanyabiashara wa dawa za kulevya.