Tanzania yaweka marufuku kwa wapenzi na wanandoa kuachana! (Video)

"Ulivyomchukua siku ya kwanza ziwa limesimama sasa hivi kazaa haliwezi kusimama tena, wewe vipi? Mkae mlee watoto."

Muhtasari

• Pia RC huyo alisema hatua kali za kisheria ikiwemo kuwafikisha kwenye vyombo vya dola vijana ambao watabainika kushindwa kulea watoto wao.

RC wa Rukwa Bi Queen Sendiga.
RC wa Rukwa Bi Queen Sendiga.
Image: Screengrab

Mkuu wa mkoa wa Rukwa nchini Tanzania kwa jina Bi Queen Sendiga ametangaza marufuku kwa wapenzi au wanandoa kuachana pindi wanapoafikiana kuanza kuishi pamoja.

Katika video moja ambayo imeenezwa mitandaoni inamuonesha Bi Sendiga akiwahutubia wananchi kwenye mkutano, alitoa agizo kwa serikali za vijijini kuwachukulia hatua wale ambao wanaoana na kisha kuachana.

Pia RC huyo alisema hatua kali za kisheria ikiwemo kuwafikisha kwenye vyombo vya dola vijana ambao watabainika kushindwa kulea watoto wao na kuzitelekeza familia zao majumbani zitachukuliwa dhidi yao.

“Ninataka nitoe maelekezo kabisa kuanzia serikali za vijiji, kijana au baba atakayepelekwa pale kwa ofisi kwa tuhuma za kukosa kulea mtoto wake tutakunyorosha vilivyo. Umetia mimba, lea mtoto wako. Na ni marufuku kuachana. Uliye naye sasa hivi vile ulivyopatana naye siku ya kwanza utajijua mwenyewe. Kamatana naye kwa faida ya watoto wako,” alisema huku akishangiliwa na watu.

Alitoa onyo kali kwa wanaume akisema kuwa wao ndio wenye mazoea ya kuacha wanawake na kuwabadilisha kama nguo.

“Sio unajifanya siku mbili tatu mwanamke huyu simtaki. Ulivyomchukua siku ya kwanza ziwa limesimama sasa hivi kazaa haliwezi kusimama tena, wewe vipi? Mkae mlee watoto kwa sababu hao watoto ndio sisi tunaowategemea kesho kutwa,” RC huyo alisema.