Tuoneshe maiti zilizokodishwa! - Wahudumu wa mochwari wamsakama IG Koome kooni

" Ofisi ya IG wa polisi ni ya kiheshima na tunashangaa jinsi ambavyo imeshushwa kiheshima kwa kauli kama hizo" katibu wa muungano wa wahudumu wa mochwari.

Muhtasari

• Wakati huo huo, mwenyekiti wa wahudumu wa mochwari Elkana Mwinani alimtaka IG Koome kukanusha kauli yake.

Aliyekuwa kamanda wa polisi wa Nairobi Japheth Koome
Image: MAKTABA

Wahuduku wa hifadhi za maiti kutoka maeneo mbali mbali nchini wamemtaka inspekta jenerali wa polisi Japhet Koome kuwaonesha maiti ambazo alidai zilikodishwa na wanaounga Azimio mkono ili kusinizia polisi kwamba ni miili ya watu ambao walidhurika mikononi mwa polisi wa kupambana na ghasia wakati wa maandamano wiki mbili zilizopita.

Siku mbili zilizopita, IG Koome katika mkutano na wanahabari alidai kwamba Azimio walikodisha maiti kutoka kwa baadho ya hifadhi za maiti nchini na kuiweka barabarani katika kile alisema kuwa ni njama ya kuipaka tope idara ya polisi kwamba ni wakatili kwa kuuwa waandamanaji waliokuwa bila silaha.

Kauli hiyo iliyotolewa na IG Koome katika chuo cha kuwafunza makurutu wa polisi Kiganjo kaunti ya Nyeri ilipokelewa kwa mshangao mkubwa na baadhi ya watu humu nchini huku viongozi wa Azimio wakiitaja kama kauli ya kipuuzi na isiyo na heshima kwa familia zilizowapoteza wapendwa wao katika maandamano hayo.

Kwa mujibu wa Felix Odhiambo ambaye ni katibu mkuu wa wahudumu wa mochwari nchini, hifadhi za maiti zinaongozwa kwa maadili na kauli ambayo IG Koome aliitoa ni ya kuwadhalilisha na hivyo kumpa changamoto ya kuwaonesha miili anayodaiwa ilikodishwa kutoka kwa mochwari.

“Wahudumu wa mochwari sio tena wakatili, walevi, wachafu na wasio na elimu. Tunafanya kazi  kwa kufuata maadili na sheria za Kenya katika kazi yetu. Ofisi ya IG wa polisi ni ya kiheshima na tunashangaa jinsi ambavyo imeshushwa kiheshima kwa kauli kama hizo. Kwa hiyo tunatoa agizo kwamba IG Koome atuoneshe maiti ambazo anadai zilikodishwa na kama itapatikana ni kweli, wahusika watachukuliwa hatua za kinidhamu,” Odhiambo alisema.

Wakati huo huo, mwenyekiti wa wahudumu wa mochwari Elkana Mwinani alimtaka IG Koome kukanusha kauli yake na kusema kwamba wao hufanya kazi yao kwa ukaribu na idara ya polisi.