Nairobi: Vilabu vya pombe vilivyopo umbali wa mita 300 kutoka kwa shule, makazi kufungwa

Maafisa wa polisi watakaopatikana wakihujumu shughuli hiyo pia watachukulia hatua za kinidhamu.

Muhtasari

• Kamishna wa kaunti ya Nairobi Katee Mwanza alisema kwamba manaibu kamishna wote wanatarajia kuorodhesha vilabu hivyo vyote.

Kunywa pombe 3 kila siku, taasisi ya magonjwa ya moyo yashauri.
Kunywa pombe 3 kila siku, taasisi ya magonjwa ya moyo yashauri.
Image: BBC

Serikali ya kitaifa imetoa agizo la kufungwa kwa baa na vilau vyote vya baa vilivyopo katika umbali wa mita 300 kutoka kwa maeneo ya makazi ya watu au shule katika kaunti ya Nairobi, gazeti la Nation limeripoti.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, agizo hili pia litalenga kuwaadhibu maafisa wa polisi ambao watapatikana kulinda vilabu hivyo kwa kuchukua hongo.

Kamishna wa kaunti ya Nairobi Katee Mwanza alisema kwamba manaibu kamishna wote wanatarajia kuorodhesha vilabu hivyo vyote kabla ya shughuli ya kuvifunga kung’oa nanga rasmi siku chache zijazo.

“Kama mnavyojua serikali ilishawahi kusema kwamba hakuna baa au klabu cha pombe kinachostahili kufanya kazi karibu na shule au makazi ya watu kwa umbali wa mita 300,” Mwanza alisema katika barua iliyoandikiwa manaibu kamishna wa Nairobi Agosti 17.

Mwanza alisema kwamba manaibu kamishna hao watatoa pia orodha fiche ya maafisa wa polisi ambao watakuwa wanalemaza shughuli hiyo kwa kulinda biashara hizo ambazo zitakuwa karibu na makazi ya watu kwa mita 300.

“Mtoe orodha ya siri ya maafisa wa polisi ambao watapatikana kuhujumu shughuli hiyo ya haramu na pia hakikisha mnapiga doria mara kwa mara ili kuhakikisha vilabu hivyo havirudii tena katika biashara hiyo haramu,” alisema.

Agizo hili linakuja miezi kadhaa baada ya suala hilo kuibuka kuwa mjadala mkali mitandaoni kufuatia baadhi ya wafanyibiashara kumenyana kwa maneno na wakaaji wa mitaa ya kifahari Nairobi ambao walikuwa wanateta kusumbuliwa na kelele kali zinazotoka kwa vilabu vilivyopo karibu na makazi yao.